Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi amesema kuwa kujifungua salama ni haki ya msingi kwa kila mwanamke hivyo Serikali inachukua hatua zote muhimu kuhakikisha haki hiyo inapatikana.

Dkt. Mwinyi ameyasema hayo wakati wa kilele cha hafla maalum ya shukrani ya kampeni ya “Uzazi ni Maisha” inayohusu kuchangia katika Mradi wa Upatikanaji wa Vifaa Tiba, ulioendeshwa na Taasisi ya Amref Tanzania katika viwanja vya Ikulu Zanzibar.

Amesema, kupitia mradi huo, Zanzibar imo katika njia sahihi ya kupunguza vifo vya mama na mtoto wakati wa kujifungua, na ameipongeza Amref kwa mafanikio makubwa yanayoendelea kupatikana.

Dkt. Mwinyi ameeleza kuwa kampeni ya “Uzazi ni Maisha” imeongeza wigo mpana kwa akina mama kujifungua salama, na watoto kuwa katika mazingira na maisha bora baada ya kuzaliwa.

Aidha, mewahakikishia wadau kuwa katika mwaka wa 2023 nchi imepata mafanikio makubwa kupitia upatikanaji wa vifaa tiba, kupitia Mradi wa Amref, kwa kufikisha huduma za matibabu katika maeneo ya mbali yenye shida ya matibabu.

Rais Dkt. Mwinyi ameahidi kuwa serikali itaendelea kuunga mkono juhudi za wadau na sekta binafsi katika kuimarisha sekta ya afya, hususan afya ya mama na mtoto.

Wahimizwa kuhamasisha uanzishwaji Vituo vya kulea Watoto