KUFA GANZI.
Kufa ganzi ni kupoteza uwezo wa kuhisi katika sehemu ya mwili wako. Huenda uwezo wako wa kuhisi ukapungua kuliko kawaida au ukakosa kuhisi kabisa. Kufa ganzi kunaweza kuwa ishara ya tatizo la ubongo au uti wako wa mgongo. Ukifa ganzi, huenda usiweze:
-
Kuhisi unapoguswa taratibu
-
Kuhisi maumivu
-
Kutofautisha joto na baridi
-
Kuhisi mtetemo
-
Kujua sehemu ya mwili wako iliyokufa ganzi
Pamoja na kufa ganzi, unaweza pia:
-
Kuwashwa au kupata hisia ya kudungwadungwa
-
Udhaifu
-
Kupooza (matatizo ya kusogeza sehemu ya mwili wako)
Kufa ganzi kunaweza kusababisha matatizo ya kuwa imara na kudhibiti mwendo. Kunaweza kuathiri uwezo wako wa kutembea au kuendesha gari.
SABABU.
Unapogusa kitu kwa mkono wako, neva zilizo kwenye mkono wako hutuma ujumbe kwa ubongo wako. Ujumbe huo hukuwezesha kuhisi kitu unachogusa. Neva sawa na hizo huunganisha sehemu zote tofauti za mwili wako kwenye ubongo wako. Tatizo la kufa ganzi hutokea wakati kuna hitilafu kwenye njia ya neva ambayo ujumbe huo husafirishwa. Magonjwa na dawa nyingi tofauti zinaweza kuzuia au kuweka shinikizo kwenye njia hii, kama vile:
-
Maambukizi, kama vile ugonjwa wa Lyme au virusi vya UKIMWI
-
Kutokuwa na vitamini B12 ya kutosha mwilini
-
Ugonjwa wa Kudhoofika kwa viungo unaoshinikiza neva zinazotoka kwenye uti wa mgongo
-
Shinikizo kwenye neva kutokana na miendo inayojirudia au kukaa katika mkao mmoja kwa muda mrefu mno
-
Majeraha kwenye ubono, uti wa mgondo au neva
Baadhi ya watu hufa ganzi na kuwashwawashwa kwenye mikono na karibu na mdomo wanapohisi wasiwasi na kupumua kwa haraka sana (kupumua kwa kasi). Hali hii si hatari.
USHAURI.
Nenda kwa daktari mara moja ikiwa una tatizo la kufa ganzi pamoja na dalili yoyote kati ya ishara hizi za tahadhari:
-
Tatizo la kufa ganzi lililokuja ghafla (ndani ya dakika au saa chache)
-
Pia una udhaifu katika sehemu ya mwili wako ambao unakuja kwa haraka (ndani ya saa au siku chache)
-
Hali ya kufa ganzi au udhaifu umeenea kwa haraka kuelekea juu au chini kwnye mwili, na kuhusisha sehemu zaidi na zaidi za mwili wako
-
Mguu au mkono mzima umekufa ganzi
-
Uso na pingiti zimekufa ganzi
-
Una tatizo la kufa ganzi au udhaifu na matatizo ya kutembea, kuzungumza au kuona
-
Mapaja, makalio, au sehemu zao za siri zimekufa ganzi na unashindwa kuzuia haja (kushindwa kuzuia mkojo au kinyesi kutoka)
-
Hali ya kufa ganzi inapatikana kwenye pande zote mbili za mwili wako chini ya sehemu mahususi, kama vile chini ya sehemu ya katikati ya kifua
Ikiwa una hali ya kufa ganzi bila ishara hizi za tahadhari, mpigie simu daktari wako. Daktari wako ataamua wakati wa kukuona kulingana na dalili zako.
TIBA.
Madaktari hutibu tatizo linalosababisha ufe ganzi.
Madaktari wanaweza kupendekeza njia za kusaidia kupunguza dalili zako na kuzuia matatizo mengine:
-
Ikiwa mguu wako umekufa ganzi, vaa viatu na soksi zinazokutoshea vizuri na uangalia kama kuna changarawe au vitu vingine ndani kabla ya kuzivaa
-
Angalia sehemu zako zilizokufa ganzi ili uone kama kuna vidonda, wekundu au kuvimba
-
Ikiwa mkono wako umekufa ganzi, kuwa mwangalifu unapogusa vitu ambavyo huenda ni moto au vina ncha kali
-
Ikiwa una matatizo ya kutembea, kupata tiba ya mazoezi au kutumia fimbo au kifaa cha kutembelea kunaweza kukusaidia kutembea kwa njia salama na kuzuia kuanguka
Zungumza na daktari wako kuhusu iwapo ni salama kwako kuendesha gari