Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), imewataka wakaguzi wa ndani wa Taasisi za Umma kuzingatia weledi wa taaluma yao ili kuleta ukidhi wa Sheria katika Ununuzi wa Umma.

Wito huo, umetolewa na Mkurugenzi Mkuu wa PPRA, Dennis Simba wakati akifungua mafunzo ya matumizi ya mfumo wa NeST katika ukaguzi wa michakato ya Ununuzi wa Umma hii leo Machi 10, 2025 katika Ukumbi wa Mikutano wa Saint Gasper Jijini Dodoma.

Amesema, wakaguzi wa ndani wamepewa jukumu nyeti sana la kuhakikisha michakato ya ununuzi inaendeshwa kwa mujibu wa Sheria na kanuni zilizowekwa na Serikali pamoja na kuandaa ripoti sahihi zinazoonesha mapungufu na mapendekezo ili kufanya maboresho katika sekta ya ununuzi.

“Kila mkaguzi wa ndani akitekeleza jumukumu lake ipasavyo, uzingatiaji wa Sheria ya Ununuzi wa Umma utaongezeka na thamani ya fedha itapatikana katika ununuzi unaofanywa na Serikali yetu,” amesema Simba.

Simba pia ametoa wito kwa Wakaguzi wote nchini pamoja na Taasisi Nunuzi zote kuendelea kutoa ushirikiano kwa Serikali ya awamu ya sita na PPRA kwa kuendelea kutumia Mfumo wa NeST katika uendeshaji wa michakato yote ya Ununuzi wa Umma.

“Nitoe rai kwenu, kuutumia vizuri mfumo huu (NeST), kwani ni nyenzo muhimu kwenu na umerahisisha upatikanaji wa taarifa kwa ajili ya shughuli zenu za ukaguzi,” amehitimisha.

Mafunzo hayo yaliyojumuisha zaidi ya washiriki 200 kutoka taasisi 91 zilizopo mkoani Dodoma, yanatarajiwa kuendeshwa kwa muda wa siku 5 kuanzia leo Machi 10, 2025 na kufikia tamati Machi 14, 2025.

Wizara ya Afya yathibitisha visa viwili vya mpox nchini