Operesheni ya siku 11 katika mikoa sita ya kanda ya ziwa, imefanikiwa kuwakamata watuhumiwa 504 wakiwemo watuhumiwa waliokiri kuhamasisha vitendo vya ubakaji na mauaji ya wanawake 29 ili wapate utajiri mkoani Tabaora.

Msako huo ulianza februari 3 mwaka huu, hadi jana ulifanikiwa kukamata watuhumiwa wa makosa mbalimbali yakiwemo matukio ya mauaji kwa kuwakata mapanga vikongwe kwa imani za ushirikina.

Wapo waliokamatwa kwa mauaji ya visasi, uendeshaji mtandao wa waganga wa kienyeji, na wapo waliokiri kuhusika kuhamasisha mauaji ya wanawake takribani 29 kwa kuwabaka kisha kuwaua ili kupata utajiri.

Mkuu wa operesheni wa jeshi la polisi nchini, kamishna msaidizi, Mihayo Msikhela katika taarifa yake kwa waandishi wa habari amesema kuwa msako huo ni endelevu na ni kutekeleza agizo la mkuu wa jeshi la polisi  nchini (IGP), Simon Siro alilolitoa Januari 20 mwaka huu.

Kwa mujibu wa kamanda Msikhela vyanzo vya mauaji hayo ni pamoja migogoro ya aridhi, imani za kishirikina, wivu wa kimapenzi, kuwania mali na kulipiza visasi ambapo ameonya kuwa hakuna mtu aliyetenda uhalifu huo atakayesalimika.

Miongoni mwa watuhumiwa waliokamatwa ni pamoja na watuhumiwa 44 wa mauaji ya kukata watu mapanga, ramli chonganishi 75, kufanya uganga bila kibali 170, unyang’anyi kwa kutumia silaha 5, waliopatikana na nyara za Serikali 33 na wizi wa mifugo 16.

Tamko la Waziri Ummy wanafunzi kutibu wagonjwa Mloganzila
Video: Tundu Lissu aibua mapya ughaibuni, PM: Msigeuze Corona kuwa mtaji wa kisiasa