Diapora kutoka nchini Canada, ambaye pia ni mwekezaji aliyeonesha nia ya kuwekeza katika miundombinu ya barabara nchini Joseph Katallah amekutana na uongozi wa Wakala wa Barabara Nchini (Tanroads) na kujadiliana nao kuhusu matumizi ya teknolojia mpya ya ujenzi wa barabara.

Katallah anashirikiana na Kampuni ya Geopolymer Solutions LLC ya Marekani inayomilikiwa na Bw. Rodney Zubrod ambayo imebuni teknolojia mpya ya ujenzi wa barabara za lami na madaraja.

Akiongea katika kikao kilichofanyika leo Jijini Dar es Salaam, baina ya Geopolymer Solutions LLC na Tanroads Bw. Katallah amesema kuwa teknolojia hiyo hutumia mabaki ya uchafu wa migodini na viwandani hususan viwandani vinavyotengeneza alumina na vioo ni nzuri na hulinda mazingira.

“Tunashukuru kupata nafasi hii kuweza kupata nafasi ya kushirikiana na Tanroads katika majadiliano ya awali, mwitikio ni mkubwa na tunaendelea na majadiliano na tunaamini teknolojia hii itasaidia kupunguza gharama pamoja na kutunza mazingira,” amesema Bw. Katalla

Kwa upande wa Kaimu Mtendaji Mkuu – Tanroads Mhandisi Nkolante Ntije amesema wamekuwa na kikao kizuri na wamesikiliza uwasilishaji wa Geopolymer Solutions LLC na kuona kuna uwezekano kutumia ‘material’ hiyo na kuiwezesha serikali kupata barabara nzuri na zilizojengwa kwa gharama nafuu.

“Serikali ina taratibu zake za kufanya utafiti kwa teknolojia yoyote mpya kabla ya kuanza kuitumia na baada ya utafiti na kujiridhisha kuwa teknolojia hiyo ni nzuri tunaamini tutakuwa tumepata jambo nzuri ambalo nchi yetu inaweza kuitumia teknolojia hiyo na kupunguza gharama katika ujenzi wa barabara kwa sababu miundombinu katika nchi yetu inahitajika sana,” amesema Mhandisi Ntije.

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kupitia idara ya Diaspora imeendelea kuwahamasisha Diaspora wengine wenye malengo ya kuwekeza katika sekta mbalimbali nchini na inawahakikishia ushirikiano katika hatua za kurasimisha uwekezaji.

Majizzo awachana wasanii waliojitoa tuzo za Muziki
Nasreddine Nabi achimba mkwara mzito Young Africans