Kiungo fundi wa mpira wa Simba SC, Saido Ntibazonkiza amesema kuwa wakati mwingine umaarufu huwa ni kama kero pale mashabiki wanapoingilia faragha za mastaa, japokuwa kama mchezaji analazimika kuzoea kwa vile anahitaji sapoti ya watu hao katika maisha ya soka.

Kauli ya Saido imekuja baada ya Saido kuvamiwa na shabiki alipotimba kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es salaam kushuhudia chama lake la zamani Geita Gold likivaana na KMC na kutoka na ushindi wa mabao 2-0, ambapo licha ya kujichanganya na watu ili asijulikane mashabiki wali- baini na kumvaa alipokuwa akitoka uwanjani hapo.

Akiwa hana hili wala lile, ghafla Saido alijikuta akivamiwa na shabiki huyo aliyekuwa na nia ya kutaka kumkumbatia, huku Mwanaspoti likishuhudia lakini staa huyo akawahi kumzuia akimtaka kwanza ajitambulishe.

Shabiki huyo aliyekuwa akizungumza Kiswahili na Kilingala alipiga magoti, huku akimuomba msaada wa pesa na katika kuepusha mambo mengi, Saido alitoa noti ya Sh5,000 na kumpa licha ya kuombwa Sh2,000.

Baada ya kupewa pesa shabiki huyo aliyeonekana kama aliyelewa aliendelea kumng’ang’ania akitaka kumkumbatia, mara apige magoti kama vile anataka kusujudia, lakini ghafla alibadilika na kuanza kumwambia amuombee, lakini staa huyo alimzuia.

Na alipopata upenyo wa kumwambia Saido ya moyoni, alisema: “Napenda mnavyocheza watatu hasa pasi ianzie kwa Chama, uipokee wewe na kisha uitoe kwa Baleke fundi wa kucheka na nyavu. Mkipangwa wote nakuwa na amani ya kupata matokeo ya ushindi,”

alisema shabiki huyo aliyejitambulisha kuwa ni mnazi mkubwa wa Simba.

Baada ya sekeseke hilo, Saido aliliambia Mwanaspoti: “Naheshimu wanaotusapoti kwenye kazi zetu, ila kuna wakati zinatokea changamoto.”

Chanzo: Mwanaspoti

Habari Kuu kwenye magazeti ya leo Aprili 14, 2023
Marco Reus kulamba dili la Euro Milion 7