Licha ya ushindi wa 2-0 dhidi ya Rivers United ya Nigeria, Kocha Mkuu wa Young Africans, Nasreddine Mohamed Nabi amesema bado ana kazi ya kufanya ili kufanikisha ndoto za kutinga Nusu Fainali ya Kombe la Shirikisho Barani Afrika.

Young Africans itakua mwenyeji wa mchezo wa Mkondo wa Pili utakaopigwa Jumapili (April 30), katika Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam.

Nabi amesema anaamini Rivers United itacheza kufa na kupona katika mchezo ujao, hivyo atahakikisha anapanga vizuri karata zake ili kulinda ushindi huo pamoja na kusaka ushindi mwingine katika mchezo wa Mkondo wa Pili.

Hata hivyo Kocha huyo kutoka nchini Tunisia amesema anashukuru kilichowapeleka nchini Nigeria amekifanikisha na alidhamiria kuwashangaza wenyeji wao, ambao kabla ya mchezo wa jana Jumapili (April 23) walikua na matumaini makubwa na kuibuka na ushindi.

“Sisi hatujaja hapa kujifurahisha, nazifahamu timu za Nigeria, kupata matokeo Nigeria ni vigumu sana, lakini tupo serious na mashindano haya. Siku zote nimekuwa nikiwaambia wachezaji wangu wajitahidi kupata matokeo mazuri ugenini kabla ya kuwaza matokeo ya uwanja wa nyumbani, ndicho hicho nilichokifanya.”

“Rivers ni timu nzuri, mashindano ya Klabu Bingwa mwaka 2021/22, Rivers walituondoa katika hatua za awali, kulikuwa na sababu nyingi lakini zaidi timu yetu haikuwa kwenye ubora tulionqo sasa hivi. Sasa hivi kikosi kipo imara na tupo tayari kupambana.”

“Sisi Waafrika tunajuana, mechi hii haijaisha, bado kuna mechi nyingine ya marudiano kwa Mkapa baada ya siku saba, kikao changu cha kwanza na wachezaji wangu itakuwa ni kuwasisitiza hilo. Nawaheshimu Rivers, kocha na wachezaji wao wote ni wazuri, lakini sisi tuna malengo ya kufika mbali zaidi kwenye mashindano haya,” amesema Nabi.

Mabao ya Young Africans katika mchezo huo uliopigwa kwenye uwanja wa Godswill Akpabio mjini Uyo, yalifungwa na Mshambuliaji kutoka DR Congo Fiston Mayele dakika ya 73 na 81.

Serikali yaishukuru DataVision ufadhili mkopo wa Kopafasta
Simon Msuva: Msimu ujao utakuwa bora zaidi