Mshambuliaji kutoka Ubelgiji Romelu Menama Lukaku anatarajiwa kupewa mkataba wa miaka miwili wenye thamani ya Pauni milioni 43 kutoka kwa miamba ya Saudi Arabia, Al-Hilal msimu huu wa joto, kwa mujibu wa ripoti.

Iwapo ofa hiyo itakubaliwa, hatua hiyo itamfanya Lukaku kuwa nyota wa hivi karibuni zaidi kujiunga na Ligi Kuu ya Saudi Arabia (Saudi Pro League) tangu fowadi Cristiano Ronaldo, ambaye alishirikiana na Al-Nassr kufuatia kuondoka kwake Manchester United Desemba mwaka jana.

Muda wa mkopo wa Mbelgiji huyo katika timu iliyomaliza nafasi ya pili kwenye Ligi ya mabingwa Ulaya, Inter Milan, utafikia tamati msimu huu wa joto, huku Lukaku akitarajiwa kuungana tena na Chelsea chini ya kocha mkuu mpya Mauricio Pochettino.

Mshambuliaji huyo aliondoka Stamford Bridge chini ya hali mbaya baada ya kuwaambia kwamba angependa kuondoka kwa zaidi ya miezi sita baada ya uhamisho wake wa pauni milioni 98 kwenda London Magharibi mnamo Agosti 2021.

Inasemekana kwamba Lukaku alikutana na maofisa wa Al-Hilal kujadili mkataba huo nchini Saudi Arabia siku ya Jumatatu, ingawa inaaminika kuwa atalipa kisogo soka la Ulaya kwa ofa nono zaidi. Kwa mujibu wa Goal.com.

Chelsea wako tayari kuachana na Lukaku lakini wanataka ada ya uhamisho ya zaidi ya Pauni milioni 43, chini ya nusu ya ile waliyolipa misimu miwili iliyopita.

Ripoti hiyo imedai kuwa Al-Hilal wanasita kulipa bei inayotakiwa na The Blues hao na watajadiliana na mwenyekiti wa Chelsea, Todd Boehy katika jitihada za kupun guza ada hiyo.

Vinara hao wa Stamford Bridge wanajiandaa kukifanyia marekebisho kikosi chao kabla ya msimu ujao kufuatia kampeni mbaya, baada ya kumaliza katika nafasi ya 12 kwenye Ligi Kuu ya England na kushindwa kufuzu kwa michuano ya Ulaya.

Ronaldo alifungua kinyang’anyiro cha nyota wa Ulaya kujiunga na ligi ya Saudi Pro League, akikubali dili nono lenye thamani ya Pauni milioni 173 kwa mwaka na Al-Nassr Januari mwaka huu.

Karim Benzema alikatisha maisha yake ya miaka 14 katika klabu ya Real Madrid ili kusaini mkataba wa Pauni milioni 86 kwa mwaka na mabingwa wa Saudia Al-Ittihad, na kiungo wa Chelsea, N’Golo Kante yuko tayari kusaini mkataba na klabu hiyo.

Afukuzwa kazi, aanika mazito ya mumewe aliyemkimbia
Vitambulisho vya NIDA kugawiwa kabla ya 2024