Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa nchini (TPBRC) imetoa onyo kali kwa waandaaji wa mapambano ya ngumi (mapromota) ambao wanaandaa mapambano bila kuwalipa mabondia stahiki zao.

Onyo hilo limetolewa na Rais wa Kamisheni hiyo Chaurembo Palasa ambapo amesema ‘Promota’ atakayebainika kutomlipa bondia atafungiwa pamoja na kutozwa faini.

“Promota hawezi kuchezesha pambano bila kumpa pesa bondia na akikiuka kanuni na taratibu atachukuliwa hatua, hii tunawakumbusha wale wote wanaoandaa mapambano ya ngumi kuhakikisha wanamalizana kwanza na mabondia,” amesema Palasa.

Aidha aamesema bondia ambaye atachukua pesa na kutopanda ulingoni malalamiko hayo yakiwafikia atampelekwa kamati ya nidhamu ambayo itampa adhabu ikiwa pamoja na kufungiwa kucheza ngumi ndani na nnje ya nchi.

Palasa amesema kwa sasa mabondia wengi wanalipwa fedha nyingi tofauti na miaka iliyopita na hii inatokana na mchezo huo kuanza kupata umaarufu mkubwa.

“Kwa sasa mchezo wa ngumi upo juu na ndio maana tunaona mabondia wengi miaka ya sasa wanafaidika kwa kiasi kikubwa kwani wanapomaliza mapambano wanalipwa kiasi kikubwa cha pesa tofauti na walivyokuwa wanalipwa miaka ya nyuma,” amesema Rais Palasa.

Fidia ya ardhi: Majaliwa aziagiza Halmashauri
Fahamu tofauti ya Eid al Adha, Eid al Fitr