Waziri wa Maliasili na Utalii, Angellah Kairuki amekutana na kufanya mazungumzo na Rais ambaye pia ni Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Utalii Duniani (World Travel Tourism Council – WTTC), Julia Simpson kwa lengo la kujadili namna bora ya kushirikiana katika kutangaza na kukuza utalii endelevu nchini Tanzania.

Kikao hicho kilifanyika jijini Riyadh, Saudi Arabia ambapo Tanzania ikiwa mwanachama wa WTTC itaendelea kujitangaza Kimataifa na kupata fursa ya kuwa mjumbe katika nafasi mbalimbali huku Baraza hilo likiwa na mtandao wa mashirika binafsi zaidi ya 200 Duniani, wanaotoa huduma mbalimbalia zenye lengo la kukuza utalii.

Aidha, katika kuendelea kutangaza utalii na kutafuta masoko mapya ya utalii, Kairuki amefanya mazungumzo na wadau wakubwa wa utalii duniani ikiwa ni pamoja na Meneja Masoko wa Shirika la Ndege la Saudi Arabia, Abdulrahman Alabdulwahab kwa lengo la kuangalia namna bora ya kuitangaza Tanzania kupitia ndege za shirika hilo na kushirikiana katika kutangaza vivutio vya Utalii nchini.

Pia, amekutana na Mkurugenzi Mkuu wa City Sightseeing World wide, Enrique Ybarra kwa lengo la kuangalia namna bora ya kuweka matangazo ya vivutio vya Tanzania kwenye vyombo vyake vya usafiri, na katika tovuti maarufu duniani ijulikanayo kama Isango.

Akiba fedha za Kigeni: BoT kununua tani sita za Dhahabu
Wimbi la uhamiaji lazidi kuitikisa Dunia - UNHCR