Shirikisho la Soka Afrika (CAF) limevithibitisha viwanja 36 vitakavyoweza kutumika kwenye mechi za hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika ukiwemo Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam.

Katika orodha hiyo ya CAF rasmi Simba SC na Young Africans zitarudi Uwanja wa Mkapa baada ya kutumia Uwanja wa Azam Complex kwenye mechi za Hatua ya mtoano.

Yanga ilitumia Uwanja wa Azam kwenye mechi zake mbili dhidi ya ASAS ya Djibouti na El Merreikh ya Sudan huku Simba SC ambayo ilianzia hatua ya kwanza ya mtoano ikitumia uwanja wa huo kwa mchezo mmoja pekee dhidi ya Power Dynamos ya Zambia.

Habari njema kwa Simba SC na Young Africans ni kwamba katika mechi zao tatu kwa kila moja za ugenini watatumia uwanja wenye nyasi halisi kulingana na viwanja vya wapinzani wao vilivyopitishwa.

Mabingwa wa Tanzania Young Africans ambao wako kundi D wapinzani wao CR Belouizdad ya Algeria nchi yao imepitishiwa viwanja vitano ambavyo ni 5 Juillet 1962, Complexe Olympique d’oran, Chahid Hamlaoui, Neslon Mandela na 19 Mai 1956.

Bingwa mtetezi Al Ahly ya Misri, nchi yao imeidhinishiwa viwanja sita ambavyo ni Cairo International, June 30, Borg El Arab, Suez, Suez Canal Authority, Al Salaam huku  Medeama ya Ghana wao wamepewa Uwanja mmoja wa Baba Yara Sports.

Simba wao ambao wako Kundi B wapinzani wao Wydad ya Morocco wamepitishiwa viwanja vitatu vya Mohamed V, Grand Marrakech, Grand Agadir. ASEC Mimosas ya Ivory Coast wao wamepewa viwanja vitatu vya Yamoussoukro, Paix de Bouake, Laurent Pokou de San – Pedro huku Jwaneng Galaxy wakipitishiwa Uwanja mmoja pekee wa Obedi Itani Chilume.

Shida ya Maji: Wasimamisha msafara na ndoo kichwani
Ujenzi Hospitali ya Wilaya Sumbawanga watiliwa shaka