Nyota wa Singida Big Stars Mkenya, Duke Abuya amesema licha ya mwenendo wa timu hiyo ila bado anaamini wana kikosi bora cha ushindani.

Kauli ya nyota huyo imekuja baada ya timu hiyo kulazimishwa sare ya mabao 2-2 na Ihefu FC juzi Jumatano (Novemba Mosi) katika Uwanja wa Liti mjini Singida na kufikisha michezo miwili mfululizo bila ya ushindi tangu mara ya mwisho ilipoifunga Namungo mabao 3-2, Oktoba 21.

“Ni wakati wa sisi wachezaji kujiangalia wenyewe na kupambana ingawa huwezi kuacha kutoa pia pongezi kwa wapinzani wetu kutokana na changamoto za kiushindani wanazotupatia, naamini tutarejea kwenye mstari mzuri,” amesema.

Duke aliyesajiliwa akitokea Police FC ya Kenya msimu huu aliongeza matokeo ya mchezo huo wameachana naya na sasa nguvu zao kubwa wanazielekeza katika mechi nyingine ngumu dhidi ya Mashujaa FC itakayopigwa Novemba 6, Uwanja wa Lake Tanganyika mkoani Kigoma.

“Kila mchezo ni mgumu lakini maandalizi bora siku zote ndiyo yanayoamua, kwetu ni changamoto nyingine iliyopo mbele yetu ambayo tunakabiliana nayo, tunawaheshimu wapinzani wote ingawa kila mechi kwetu tutaicheza kama fainali kuanzia sasa.”

Romelu Lukaku aiibua tena Inter Milan
Manchester United yajisogeza kwa Sacha Boey