Balozi wa Norway Tanzania, Tone Tinnes amewataka wadau wa kutetea masuala ya wanawake na uongozi pamoja na ushiriki katika demokraisia kuwekeza katika mbinu za kukabiliana na vitendo vya ukatili kwa wanawake vinavyowakwamisha kufikia malengo ya kushika nafasi za uongozi katika ngazi mbalimbali.

Balozi Tinnes amesema hayo wakati aliposhiriki mdahalo wa kitaifa wa wadau wa kutetea masuala ya wanawake na uongozi pamoja na ushiriki wao katika demokrasia Zanzibar ulioandaliwa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania, Zanzibar – TAMWA ZNZ, Jumuiya ya Wanasheria Wanawake Zanzibar – ZAFELA na Jumuiya ya utetezi wa Jinsia na Mazingira Pemba – PEGAO, kwa kushirikiana na Ubalozi wa Norway Tanzania.

“Ajenda ya 50/50 ni ajenda ya kidunia, hivyo ni muhimu kuangalia jinsi gani kama wadau tunaweza kukabiliana na ukatili wa kijinsia kwa wanawake ili waweze kushika nafasi za uongozi. Majukwaa kama haya ya kujadili masuala ya wanawake na uongozi ni muhimu hasa tunapojipanga kuelekea uchaguzi wa mwaka 2025, na kuna changamoito nyingi hasa ukatili na udhalilishaji wa kijinsia,” amesema Balozi Tinnes.

Alisema, mdahalo huo uliolenga kujadili hali ya wanawake na uongozi Zanzibar katika siku 16 za kupinga ukatili kwa wanawake na watoto, alisema ajenda ya usawa wa kijinsia ni muhimu ukatiliwa mkazo na wadau wote ili kuhakikisha lengo linafikiwa na kwamba kujadili nafasi ya wanawake na vikwazo vinavyowakabili navyo katika uongozi ni muhimu katika kuwajengea uwezo wanawake kujitayarisha hasa kuelekea uchaguzi mkuu wa Tanzania wa mwaka 2025.

Aidha Balozi huyo alieleza kuguswa na juhudi za TAMWA Zanzibar za kutetea haki za wanawake katika kupinga vitendo vya ukatili Zanzibar, na kueleza kuwa Serikali ya Norway itaendelea kuunga mkono juhudi hizo ili kufikia lengo la usawa wa kijinsia na kudai kuwa, “ujumbe mkuu wa mwaka huu umetushajihisha kuwekeza katika kupinga udhalilishaji wa kijinsia, na sisi ubalozi wa Norway, tumewekeza katika kusapoti TAMWA Zanzibar kwenye kuwawezesha wanawake kuanzia mashinani.”

Katika hatua nyingine Balozi Tinnes alionesha kufurahishwa na utayari wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa kuwa mstari wa mbele kukuza kwa vitendo ushiriki wa wanawake katika nafasiza uongozi kwa kusema “nafurahi kuona viongozi wakuu wa serikali kufika hapa kwani inaonesha kuwa kama nchi wanawekeza katika kukuza usawa wa kijinsia, ikiwemo nafasi na uongozi Kwa wanawake.”

Awali, Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsi, wazee na Watoto Zanzibar, Anna Athanas Paul, alibainisha kuwa Serikali inaendelea kutekeleza mkakati muhimu wa kuwawezesha wanawake katika nyanja mbalimbali kwa mjibu wa mikataba ya kikanda na kimataifa.

Alisema, “Serikali ya Mapinduzi Zanzibar inaendela kutekeleza mikakati muhimu ya kuwawezesha wanawake ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa mikataba ya kimataifa na ya kikanda, na nafasi hizi si nafasi za upendeleo bali ni kuziba nafasi na mapengo ya usawa wa kijinsia iliyopo.”

Naye Katibu Mkuu Wizara ya Elimu na Mfunzo ya Amali Zanzibar (WEMA), Khamis Abdullah Said alizitaka taasisi za Serikali na kiraia kuanza kutekeleza mkakati wa usawa wa kijinsia kwa kuzingatia uwiano sawa katika nafasi zote za uongozi kwenye ngazi mbalimbali.

“kuna haja kwa taasisi za serikali na zisizo za serikali kuzingatia uwiano wa jinsia katika nafasi za uongozi, mfano mzuri ni Wizara ya elimu, mkurugenzi mtendaji, mkurugenzi elimu mbadala, muhasibu, mkaguzi mkuu na mkurugenzi wa kitengo elimu ya juu haWA wote ni wanawake,” alisema.

Alisema wizara hiyo ipo katika hatua za kurekebisha sera ya elimu, hivyo atahakikisha utekelezaji wake utazingatia na kuaksi ajeng=da ya usawa wa kijinsia kwa kutoa fursa sawa kwa wote na kuongeza, “hivi sasa tunarekebisha Sera ya elimu, na mimi nitahakikisha inazingatia uwiano wa kijinsia. Lakini pia tunatekeleza kwa vitendo ajenda hii, kwani wizara ya elimu safu ya uongozi imezingatia sana nafasi za wanawake, kwa mfano vitengo vingi vya wizara vinaongozwa na wanawake.”

Kwa upande wake Mkurugenzi wa TAMWA ZNZ, Dkt. Mzuri Issa alisema kwa kushirikiana na wadau wengine waliandaa mdahalo huo kwa lengo la kuongeza hamasa kwa wanawake kutokata tamaa na badala yake wajitokeze kugombea nafasi mbalimbali za uongozi zinapojitokeza na kwamba Wanawake katika siasa wanakabiliwa na vikwazo mbalimbali ikiwemo udhalilishaji hasa mwanamke anapoonekana kuwa ni tishio kwa wanaume.

Akiongea katika mdahalo huo, Mwakilishi Jimbo la Konde Pemba, Zawadi Amour, kupitia Chama cha Mapinduzi, akichangia mada aliwasihi wanawake kujiamini na kutokatishwa tamaa na vikwazo wanavyowekewa na badala yake wavitumie kama ngao ya kufikia ushindi wao na kuongeza kuwa, “kujiamini ni ngao ya kumvusha mwananmke na kuweza kutimiza malengo yake kwenye uongozi, ni lazima kuwa na malengo bayana na upambanie kuyatimiza.”

Mdahalo huo wa kitaifa, ulihudhuriwa na viongozi kutoka taasisi za kiserikali na asasi za kiraia, vyama vya siasa, wanafunzi kutoka vyuo mbalimbali, viongozi wa dini, vijana wa kike na wanawake kutoka maeneo mbalimbali na kupata fursa ya kujadili mbinu wezeshi za kuwasaidia wanawake kushika viti vya uongozi ifikapo uchaguzi 2025 pamoja na kubainisha njia za kuvunja vizuizi na kufungua fursa zaidi kwa wanawake na vijana.

Paul Scholes amrudisha darasani Antony
Yacouba anarejea Ligi Kuu Tanzania Bara