Kocha Mkuu wa Mtibwa Sugar, Zuber Katwila amesema usajili walioufanya kwenye Dirisha Dogo utaiondoa timu yake katika nafasi ya mwisho waliopo hivi sasa.

Baadhi ya wachezaji wazawa waliojiunga na timu hiyo ni Charles Ilamfya kutoka Ihefu FC, Jimmyson Mwanuke na Nassoro Kapama kutoka Simba.

Kocha huyo amesema tayari wamekamilisha usajili wa nyota nane wa kimataifa kutoka nchi za Kenya, Nigeria na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na wachezaji wengine wazawa.

“Kilichokuwa kinaisumbua Mtibwa tayari tumekipatia tiba sasa mashabiki wasubiri raha, tumesajili watu wa kazi na tutawatambulisha muda mfupi baada ya taratibu zao za uhamisho kukamilika ” amesema Katwila.

Katika hatua nyingine Kocha huyo ameushukuru uongozi wa Mtibwa Sugar kwa kusikiliza maombi yake na kuchukua hatua za haraka.

Amesema hadi sasa wachezaji wote wapya waliosajiliwa wapo kambini kwao Manungu wakiendelea na mazoezi, huku uongozi ukikamilisha taratibu muhimu za usajili wao na anaamini kila kitu kinakwenda vizuri.

Ally Kamwe: Tumepata mtu sahihi
Onana afafanua picha aliopigwa AFCON 2023