Kocha Mkuu wa Mbuni, Leonard Budeba amesema, licha ya kikosi hicho kufanya usajili bora kwa msimu huu ila moja ya nyota anayempa matumaini makubwa ya kufanya vizuri ni mshambuliaji, Miraji Athuman ‘Sheva’ kutokana na uzoefu aliokuwa nao.

Sheva amejiunga na timu hiyo msimu huu huku akikumbukwa zaidi baada ya kutamba na klabu mbalimbali nchini zikiwemo za KMC, Simba, Geita Gold na JKT Tanzania jambo linalomfanya Budeba kuamini atakuwa chachu ya mafanikio ya kikosi hicho.

“Tumefanya usajili mzuri kutokana na malengo tuliyojiwekea msimu huu, Ligi ya Championship ni ngumu kwa sababu kila mtu amejipanga vizuri kuleta ushindani hivyo ilitulazimu kuhakikisha tunapata wachezaji wazoefu na Sheva ni miongoni mwao.”

Budeba aliongeza, hawezi kuahidi chochote kwa sasa ndani ya kikosi hicho isipokuwa watahakikisha wanaendeleza mwenendo mzuri wa matokeo, kwa sababu msimu uliopita changamoto hiyo ndiyo iliyowakwamisha kutimiza malengo ya kupanda Ligi Kuu Bara.

Timu hiyo kutoka jijini Arusha inashiriki Ligi ya Championship kwa msimu wa tatu mfululizo, ambapo kwa msimu uliopita ilishika nafasi ya saba na pointi 42, baada ya kushinda michezo 12, sare sita na kupoteza 12 kwenye mechi 30 ilizocheza.

Huduma Bingwa: Wananchi watoa ombi, DC Kaganda awapa neno
Ziara ya kikazi Ruvuma: Rais Samia awasili Songea