Hali ya lishe nchini imeendelea kuimarika kwa kwa kuzingatia Takwimu zinaonesha kupungua kwa viwango vya utapiamlo kwa baadhi ya viashiria ikiwemo kiwango cha udumavu kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano ambacho ndio kiashiria kikuu cha utapiamlo kimepungua kutoka asilimia 32 mwaka 2018 hadi asilimia 30 mwaka 2022 (DHS 2022).

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu, Dkt. Jim Yonazi ameyasema hayo wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Kumi wa Wadau wa Lishe nchini unaofanyika Jijini Mwanza, ukiwakutanisha wadau wa afua za lishe kwa lengo la kupokea na kujadili hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa afua za lishe kwa kipindi cha mwaka wa tatu 2023/2024 katika maeneo mahsusi yaliyoanishwa kwenye Mpango Jumuishi wa Kitaifa wa Lishe (2021/22-2025/26).

Amesema, Mkutano huo unatoa fursa kwa wadau wote wa lishe kujadili namna utekelezaji ulivyofanyika, changamoto na mikakati ya kufanikisha utekelezaji katika kipindi kilichobaki cha utekelezaji wa mpango huo hususan mwaka 2025/26. Pia Mkutano huu unatazamiwa kuongeza msukumo mpya wa utekelezaji wa afua za lishe miongoni mwa wadau kama moja ya nguzo muhimu kwa maendeleo ya Taifa.

“Kiwango cha ukondefu pia kimepungua kutoka asilimia 3.8 mwaka 2014 hadi asilimia 3.5 mwaka 2018, ingawa takwimu hizi zilibadilika mwanzoni mwa mwaka 2023 baada ya kupata matokeo ya utafiti uliofanywa Machi – Julai 2022 na Taasisi ya Chakula na Lishe na Ofisi ya Taifa ya Takwimu,” alisema Dkt. Yonazi.

“Uwepo wa wadau katika mkutano huo ni uthibitisho tosha wa ushirikiano uliopo na utayari wao katika kuboresha hali ya lishe kwa Watanzania, hususan makundi yanayoathirika zaidi ambayo ni watoto wadogo na wachanga, watu wenye mahitaji maalum, wanawake wajawazito na wale walio katika umri wa uzazi,”  aliongeza.

Aidha, ametumia mkutuno huu kuiasa jamii kuendelea kushiriki kikamilifu na kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuhakikisha hali ya lishe kwa Watanzania inaendelea kuimarika huku akisema kuwa Serikali inaahidi kuendelea kuunga mkono juhudi zilizopo na nyingine za wadau ili kuhakikisha Taifa linapata mafanikio dhidi ya mapambano ya tatizo la utapiamlo.

Kwa upande wake, Waziri Mkuu Mstaafu Mizengo Pinda amesema, Serikali imeendelea kufanya kazi kubwa ya kuhakikisha jamii inaendelea na mapambano haya ya lishe duni na kuhakikisha Taifa linaendelea kuwa na watu wenye afya bora, na kukumbusha jamiii kuwa mstari wa mbele katika masuala ya afua za Lishe.

“Masuala ya lishe yawekewe mkazo zaidi kuanzia katika elimu ya msingi hasa kupitia uwepo wa Klabu maalum zinazochagiza masuala ya afua za lishe nchini lengo ni kuwajengea uelewa watoto kuwa na elimu ya kina kuhusu masuala haya,” amesema Pinda.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Anthony Mtaka ameeleza jitihada zinazofanywa na mkoa wake katika mapambano dhidi ya Utapiamlo na masuala yote ya lishe ambapo amesema ni wakati sahihi kuwa na mikakati inayotekelezeka ili kuwa na jamii yenye lishe na afya bora.

Mkutano Mkuu wa Kumi wa Wadau wa Lishe nchini umeratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania, na umebebwa na kauli mbiu isemayo “Kuchagiza Mchango wa Wadau wa Kisekta ili Kudumisha Matokeo Bora ya Hali ya Lishe Nchini Tanzania” ukilenga kufanya tathmini ya utekelezaji wa Mpango Jumuishi wa pili wa Taifa wa Lishe, ili kuendelea kukabiliana na changamoto za utapiamlo nchini.

Bashungwa amkalia kooni Mkandarasi Barabara ya mzunguko
Habari kuu kwenye Magazeti ya leo Oktoba 3, 2024