Mkurugenzi wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake – TAMWA ZNZ, Dkt. Mzuri Issa amewataka Wanawake kutumia vyombo vya Habari kuzitangaza kazi zao , hasa zile zinazohusu  mabadiliko ya Tabia nchi.

Dkt. Mzuri ameyasema hayo wakati akizungumza na Wandishi wa Habari na Wadau mbalimbali Tunguu Unguja, katika kikao cha kuandaa mwongozo wa namna gani Waandishi watashirikiana na jamii katika kuripoti habari za mabadiliko ya Tabia nchi.

Amesema, mwongozo huo utasaidia kuleta mabadiliko makubwa nchini hivyo ni vyema waandishi kuitumia elimu hiyo ili kuhakikisha mabadiliko ya  Tabia nchi yanabadilika kwa kiwango kikubwa.

Kuhusu masuala ya kijinsia katika mabadiliko ya hali ya nchi, Dkt. Mzuri aliwataka Wanawake kufanya kazi kwa kujiamini sambamba na kuondoa hofu wakati wanapotoa taarifa husika kwa vyombo vya habari.

Kwa upande wake Mkufunzi, Shifaa Said Hassan amewataka waandishi hao pamoja na wadau wa sekta mbalimbali kufanyia kazi muongozo huo kwani ukitumiwa ipasavyo,  utasaidia kuleta mabadiliko katika jamii na taifa Kwa ujumla.

Akichangia mada katika kikao hicho Mhadhiri kutoka chuo kikuu Cha Zanzibar (SUZA), Dkt. Salim Suleiman alisema muongozo wa kuwasaidia wanawake kutumia vyombo vya habari ni mzuri, lakini pia wanawake hao wafundishwe jinsi ya kuweka kumbukumbu  vizuri katika vikundi vyao.

Naye, mshiriki katika  kikao hicho Najat Omar mwandishi kutoka The Chanzo,  alisema ni vyema wanawake hao kuunda magrupu ya mitandao ya kijamii ili kuwasaidia kutuma matukio yanayotokea katika jamii ili wandishi wa habari iwe rahisi kuyaripoti.

Siku ya Kimataifa ya Mtoto wa Kike: Wadau waandaa jambo Zanzibar
Habari kuu kwenye Magazeti ya leo Oktoba 6, 2024