Elimu ya Afya, kuhusu uchukuaji wa tahadhari ya kujikinga na ugonjwa wa Marburg, imeendelea katika maeneo mbalimbali Wilayani Biharamulo Mkoani Kagera.
Akizungumza mara baada ya kutembelea na kukagua shughuli zinazofanywa na Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii katika Kijiji cha Nemba, Wilayani Biharamulo, Mkurugenzi wa Huduma za Kinga kutoka Wizara ya Afya, Dkt. Ntuli Kapologwe, amepongeza juhudi za Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii katika kutoa elimu ya Ugonjwa ya ugonjwa huo.
Dkt. Ntuli ambaye pia ni Mkuu wa Timu ya Taifa inayokabiliana na mlipuko wa Ugonjwa wa Marburg Wilayani Biharamulo, pia ametoa wito kwao kuendelea na kazi hiyo muhimu, ili kulinda afya ya jamii na kudhibiti na kutokomeza ugonjwa huo.
“Nimefanya ziara katika Kata ya Nemba kujionea namna Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii wanavyofanya kazi na kwa kweli wanafanya Kazi kubwa sana kwani Mhudumu mmoja kwa Siku anatembelea zaidi ya kaya 8 hadi 10,” amesema.
Akizungumza katika vijiji vya Miganga na Minyororo kuhakiki namna elimu ya afya kuhusu ugonjwa wa Marburg ilivyoifikia Jamii, Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Elimu ya Afya kwa Umma kutoka Wizara ya Afya Dkt. Ona Machangu ameikumbusha Jamii kuendelea kuchukua tahadhari za kiafya ikiwemo umuhimu wa kunawa mikono kwa maji tiririka na sabuni na kutoa taarifa kwa kupiga namba Bure 199.
Amesema, “namba yetu ya Wizara 199 ni muhimu sana , uonapo dalili kama Homa, maumivu ya misuli, kutapika damu na ni muhimu kunawa mikono mara kwa mara,ukitoka chooni, kabla ya kula na ukitoka kufanya shughuli mbalimbali.”