Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhandisi Hamad Yusuf Masauni amezindua Mradi wa Suluhisha ‘RESOLVE’ ambao unalenga katika utunzaji wa vyanzo vya maji, misitu na maeneo yanayohusika na shughuli za kilimo.

Mradi huo unaotekelezwa na Shirika la Kimataifa la Hifadhi ya Mazingira utatekeleza katika mikoa ya Morogoro na Iringa kwa muda wa
miaka mitatu.

Sanjari na kuzindua mradi huo Mhandisi Masauni Waziri Masauni amefunga warsha ya wadau wanaofadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Norway (NORAD), linalohusu uhusiano uliopo baina ya Mabadiliko ya tabianchi na kilimo.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, amesema Ofisi ya Makamu wa Rais itaendeleza dhamira yake ya kuunga mkono sera na programu zinazokuza kilimo endelevu na kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.

Pia, Waziri Masauni amesema Ofisi itaendelea kufanya kazi kwa karibu na wadau wote ili kukusanya rasilimali, kuimarisha uwezo na kuleta mabadiliko yenye matokeo na kufanikiwa kwa miradi iliyopo na mipya itakayoonesha dhamira katika uhifadhi na utunzaji wa mazingira.

“Kwanza kabisa, nitoe shukrani zangu za dhati kwa washiriki wote, watafiti wetu, watendaji wetu, watunga sera, wakulima na washirika wa maendeleo kwa ushiriki wenu, michango ya busara na kujitolea katika kuandaa warsha hii muhimu ya kilimo na mabadiliko ya tabianchi.

 

“Kilimo kinasalia kuwa uti wa mgongo wa uchumi wa Tanzania, kinatoa riziki kwa watu wengi na kuchangia kwa kiasi kikubwa usalama wa chakula wa Taifa na ukuaji wa uchumi. Hata hivyo, tunafahamu kikamilifu kwamba sekta hii muhimu iko hatarini zaidi kwa athari za mabadiliko ya tabianchi,” amesema.

Aidha, Masauni amesema kupanda kwa halijoto, mvua zisizo na mpangilio, ukame wa muda mrefu, na matukio mengine mabaya ya hali ya
hewa huleta tishio kubwa kwa tija ya kilimo, mifumo ikolojia na maisha ya vijijini.

Kwa upande wake, Mratibu wa mradi huo, Anthony Mhagama amesema mradi umefika wakati muhimu ambapo Tanzania kama nchi nyingine imekuwa ikikabiliwa na mabadiliko ya tabianchi, hivyo utasaidia jamii kupata mbinu za kukabiliana na changamoto mbalimbali za mabadiliko ya tabianchi.

Warsha hiyo imeangazia mambo kadhaa muhimu ya kuchukua kama vile haja ya dharura ya kujumuisha mbinu za kilimo zinazozingatia mabadiliko ya tabianchi ili kuongeza tija huku kupunguza utoaji wa gesi chafuzi.

Pia wataalamu hao waliangalia umuhimu wa kuendeleza utafiti, uvumbuzi, na uhamisho wa teknolojia ili kuwawezesha wakulima kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa pamoja na umuhimu wa uwiano wa sera na ushirikiano katika sekta zote ili kufikia malengo yetu ya pamoja.

Newcastle yatuma salamu kwa atakayetimba Fainali baada ya kumsambaratisha Arsenal
Watanzania waendelea kuaswa kuuenzi Muungano