Kamati ya Kudumu ya Bunge ya TAMISEMI, imewataka Wananchi kuacha shughuli za kilimo kando ya mto ulipojengwa Daraja la Mawe la Garkawe katika barabara ya Maretadu – Garkawe, Wilaya ya Mbulu mkoani Manyara, ili kulinda miundombinu ya daraja hilo.
Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Justin Nyamoga ametoa wito huo katika ziara ya kukagua mradi wa daraja hilo, ambalo limejengwa kwa fedha za tozo ya Mafuta kiasi cha Sh.Milioni 470.95.
Aliutaka uongozi wa Wilaya ya Mbulu kufuatilia na kuzungumza na wananchi ili kuhakikisha shughuli za kilimo haziendelei karibu na daraja hilo.
“Madaraja haya yanajengwa kwa gharama kubwa, na tunatambua kuwa wananchi wanahitaji kulima. Hata hivyo, ni muhimu kuacha nafasi ili mto huu usiendelee kupanuka, kwani inaweza kusababisha madhara kwenye daraja,” amesema Nyamoga.
Kwa upande wake, Naibu Waziri, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Zainab Katimba, akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amesema kuwa ujenzi wa madaraja ya mawe, ikiwamo la Garkawe, umesaidia kupunguza gharama za ujenzi kutokana na wepesi wa upatikanaji wa malighafi.
“Madaraja haya yaliyotumia teknolojia ya mawe yamejengwa 238 kwa gharama ya jumla ya Sh.Bilioni 12.52 nchini kote. Ni hatua kubwa katika kupunguza gharama za ujenzi na kuongeza ufanisi,” amesema Katimba.