Mwanafunzi aliyemaliza darasa la 7 wiki iliyopita katika shule ya msingi Njungwa, Kijiji cha  Ngayaki wilayani Gairo, Rahel Yohana (14), amekutwa amejinyonga hadi kufa kwa kutumia kanga huku chanzo kikitajwa ni ugomvi kati yake na mama yake mzazi aliyekuwa akimkataza kurudi nyumbani usiku.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo Kamanda wa Polisi mkoa wa Morogoro, Wilbroad Mutafungwa, amesema tukio hilo limetokea Oktoba 15 mwaka huu.

Kamanda Mutafungwa ametoa wito kwa wale watu wanaoona njia bora ya kutatua changamoto wanazokutana nazo kwenye maisha ni kukatisha uhai wao, kuwa siyo sahihi na badala yake watafute ufumbuzi wa changamoto zao kwa wataalam wa saikolojia.

“Aligombezwa na mama yake kwa kosa la kurudi nyumbani mara kwa mara usiku na alitoweka nyumbani na ndipo alipokutwa amejinyoga vichakani, nitoe wito kwa watu ambao wanafikiri ‘shortcuts’ ya changamoto wanazokutana nazo kwenye maisha ni kuamua kujinyonga, hiyo si sahihi ni bora ukutane na wataalam wa kisaikolojia ili wakusaidie”, Amesema Kamanda Mutafungwa.

Na mwili wa mtoto huyo mara baada ya kufanyiwa uchunguzi ulikabidhiwa kwa ndugu kwa ajili ya mazishi.

Habari kubwa kwenye magazeti leo, Oktoba 19, 2020
Zanzibar na Serikali ya muungano kutatua changamoto tano