Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam linawashikilia Askari wawili wa kikosi cha kutuliza ghasia (FFU) kwa tuhuma za kuwashambulia wananchi wa Ukonga jijini humo.

Askari hao wanashikiliwa na jeshi mara baada ya mkuu wa wilaya ya Ilala, Sophia Mjema kutoa agizo kwa jeshi hilo kuwasaka askari wote waliohusika katika tukio hilo la kuwapiga wananchi hao.

Aidha, akitoa agizo hilo, pia mkuu huyo wa wilaya alitoa wito kwa wananchi waliopigwa na askari hao kujiorodhesha majina yao kwenye Ofisi ya Ofisa Mtendaji Kata ili kuweza kuona namna ya kuwasaidia.

Wananchi hao wa Ukonga Mombasa waliandamana na kufunga barabara kwa madai ya kuchoshwa ma mateso ambayo wamekuwa wakiyapata ikiwemo kupigwa kutoka katika kikosi hicho kilichopo Mombasa.

Kwa upande wake Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam, Lazaro Mambosasa amesema kuwa mpaka sasa wanawashikilia askari wawili na bado linaendelea na uchunguzi

“Ni kweli tumewakamata watu wawili ambao ni askari na bado tunaendelea na uchunguzi, hivyo nitatoa taarifa kamili pindi tu tutakapokamilisha uchunguzi wetu,”amesema Kamanda Mambosasa.

Lulu akutwa na hatia ya kuua bila kukusudia, hukumu yake kutolewa Novemba 13
Chelsea yatinga robo fainali Carabao Cup, Tottenham yashindwa kutamba nyumbani