Azam FC inashusha wachezaji sita mahiri kwa majaribio ya kujiunga na kuimarisha kikosi cha msimu ujao ambacho pia kitawakilisha nchi kwenye mashindano ya CECAFA Kagame Cup wiki tatu zijazo na Kombe la Shirikisho mwakani.

Wachezaji wanaokuja kwa mazungumzo, majaribio na kupima afya zao kabla ya kujiunga na kikosi cha Stewart Hall ni pamoja na mshambuliaji anayeongoza kufumania nyavu kwenye ligi ya Zambia toka klabu ya Nkana Red Devils Jimmy Ndhlovu ambaye awali alikuwa akicheza kwa mkopo kwenye klabu ya Power Dynamos. Jimmy tayari amekuwa kwenye rada za vilabu vingi vya Afrika Kusini hasa Morroka Swallows ambao wanamnyatia hivi sasa.

Katika orodha hiyo yumo mshambulizi toka nchini Uingereza Joe Dickson ambaye kocha Stewart Hall anamfahamu vema kama ilivyo kwa kiungo mchezeshaji Ryan Burge kutoka nchini Uingereza pia.

Jean Baptiste Mugiraneza (Migi ) ni kiungo mwenye uwezo wa kucheza kwa ufasaha nafasi ya ulinzi kama ilivyokuwa kwa Mutesa Patrick Mafisango.

Kwa sasa Migi anakipiga kwenye klabu bingwa nchini Rwanda ya APR na timu ya taifa ya Rwanda Amavubi. Habari za ujio wa Migi zilikwisha vuja kwenye baadhi ya vyombo vya habari nchini Rwanda, Uganda na Tanzania na sasa klabu ya Azam FC inathibitisha kuwa mchezaji huyu wa zamani wa Kiyovu Sports FC mwenye uzoefu mkubwa na mikikimikiki ya soka la Afrika Mashariki atatua nchini baada ya kumaliza majukumu yake na timu ya Taifa ya Rwanda.

Azam FC pia inawaleta magolikipa wawili wenye uwezo mkubwa na uzoefu wa kutosha na mikikimikiki ya soka la Afrika ili kwenda sambamba na vilabu vinavyotamba barani Afrika. Wachezaji hao ni Vincent Atchouailou De Paul Angban kutoka klabu ya Juanesse ya kwao Ivory Coast na mlinda lango Mcameroon Nelson Bongaman toka DCMP ya Kishasa DRC.

Stars Ya Mkwasa Kuelekea Uganda Siku Mbili Zijazo kuivaa ‘The Cranes’
Tetesi za ‘Nyerere kumkataa Lowasa’ zajibiwa