Siku chache baada ya kuachia video ya wimbo wake – ‘NINGEFANYAJE’, mkali wa R&B kutoka Tanzania, Bernard Paul maarufu kama Ben Pol ameeleza sababu zilizopelekea muimbaji Avril kutoka Kenya aliyeshirikishwa kwenye wimbo huo, kutoonekana kwenye video hiyo anayoitaja kuwa kubwa kuliko video zote alizowahi kufanya.

Katika video hiyo iliyoongozwa na Justin Campos wa Afrika Kusini, Ben Pol anaonekana akiimba na Rossie M ambaye pia ameshirikishwa kwenye wimbo huo huku mashabiki wakiisikia sauti ya Avril bila kumuona mwimbaji huyo mrembo.

Ben Pol amewaomba radhi mashabiki wake kwa kuwapa video ambayo haijakamilisha wahusika wote hususan kutokuonekana kwa Avril, na kwamba sababu zilizopelekea hivyo zilikuwa nje ya uwezo wa pande zote katika utayarishaji wa video hiyo.

Ben amesema kuwa baada ya yeye na Rossie M kuwasili Afrika Kusini ilikoshutiwa video hiyo zilijitokeza changamoto muda mfupi kabla ya kuanza zoezi hilo. Ben Pol ameeleza kuwa pamoja na kuwa na maandalizi makubwa, video ya ‘Ningefanyaje’ ilikumbwa na changamoto nyingi tangu awali zilizopelekea kuahirishwa mara tatu. “Kwa kweli hii video tokea mwanzo ilikuwa na changamoto, kwanza tuliisogeza mbele karibu mara tatu tena tukiwa tayari tumeshafika Afrika Kusini mimi na Rossie,” alisema Ben Pol. “Mara ya kwanza ni kutokana na ‘delay’ ya viza upande wa Avril. Si unajua Wakenya wao wanaenda South kwa viza tofauti na sisi Tanzania hatuendi kwa viza so kwetu ni rahisi zaidi muda wowote tu ukiamua fasta unaenda,” aliongeza.

Mkali huyo alieleza kuwa baada ya terehe mpya kupangwa na muongozaji aliyeshuti video hiyo, Justin Campos siku moja kabla ya kushuti AVRIL akapata tatizo lingine ambalo lilimzuia kusafiri kwa siku iliyofata kwenda Afrika Kusini. Wakati huo huo, Campos naye alimueleza Ben Pol kuwa kwa jinsi ratiba yake ilivyo endapo ataahirisha tena kushuti video hiyo, ratiba yake isingemruhusu kushuti video hiyo hadi Januari au Februari 2016, kitu ambacho Ben Pol amesema kisingewezekana kwasababu ingeendelea kumgharimu zaidi kifedha na kuvuruga ‘timing’ yake. “Kutokana na hali hiyo, sikuwa na jinsi nyingine zaidi ya kukubali matokeo kwasababu mwisho wa siku si mimi wala Avril wala director aliyekwamisha bali ni ‘situation’ ambayo ilikuwa nje ya uwezo wa kibinadamu.” Ben Pol anaeleza.

Ameongezea kuwa pamoja na kwamba angeweza kuamua kushuti video kwa kutumia version nyingine ya wimbo huo isiyokuwa na sauti ya Avril ili video isionekane na upungufu wake, lakini hakupenda kufanya hivyo kwa kuwa lengo kuu la wimbo lilikuwa kumshirikisha mwimbaji huyo. Pia, mashabiki wangekosa ladha nzuri na kazi nzuri aliyoifanya Avril. Hivyo, aliamua kufanya video hiyo bila Avril na kukusudia kuwaeleza mashabiki wake kilichosababisha hali hiyo kwa kuwa aliamini mashabiki wataelewa magumu aliyopitia katika kuwapa video hiyo waliyokuwa wakiisubiri.

“Namshukuru sana Avril kwa kukubali kufanya kazi na mimi kwasababu imetimiza moja kati ya malengo yangu ya 2015, ambayo ilikuwa kuanza kufanya kazi na wasanii wa nje ya Tanzania na yeye ndiye alikuwa chaguo langu la kwanza. Ni imani yangu tutafanya tena project nyingine ya pamoja na kuikamilisha kama tulivyoikusudia,” alimaliza Ben Pol na kuwashukuru mashabiki wake kwa kuupokea kwa mtazamo chanya wimbo na video yake.

CCM Yajipanga Kumpiku Maalim Seif Zanzibar na CUF
Museveni Kujaribu Kuiokoa Burundi Kuanzia Kesho