China na Russia zilitumia siku ya pili ya Mkutano wa BRICS wa nchi zinazoibukia kiuchumi, kuzikosoa nchi za Magharibi, huku pia zikiunga mkono mapendekezo ya upanuzi wa kile kinachoonekana na wengine, kama kundi mbadala lenye nguvu duniani.

Viongozi wa Brazil, Russia, India, China na Afrika Kusini walifanya mazungumzo ya faragha juu ya uwezekano wa upanuzi wa muungano wao wa kiuchumi wa BRICS, hatua ambayo wanasema ni njia ya kuinua sauti ya mataifa yanayoendelea, lakini ambayo pia inatumika kwa maslahi ya kisiasa ya Beijing na Moscow.

Akizungumza kwa njia ya video, Rais wa Russia Vladmir Putin ambaye aliamuru uvamizi wa Russia nchini Ukraine mwaka jana alisema hatua za nchi za Magharibi zimesababisha mzozo huo kwa kujaribu “kuonyesha ushujaa wao,” “upekee,” na sera za “ukoloni mamboleo.”

Naye Kiongozi wa China Xi Jinping alisema kuwa dunia ilikuwa katika mabadiliko makubwa na imeingia katika kipindi kipya cha “msukosuko na mabadiliko.” Alilaumu nchi zinazounda “makundi maalum” kwa tatizo hilo.

Uamuzi wa kama kukubali wanachama wapya ulitarajiwa Jumatano jioni, siku ya pili ya mkutano wa siku tatu wa BRICS mjini Johannesburg. Lakini maafisa walisema hilo lilionekana klama halitafanyika Jumatano, na tamko linaweza kutolewa Alhamisi.

Rais wa China Xi Jinping, Rais wa Brazil Luiz Inacio Lula da Silva, Waziri Mkuu wa India Narendra Modi na Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa, walikutana katika ukumbi wa mikutano katika wilaya ya kifedha ya Sandton katika jiji hilo kubwa zaidi la Afrika Kusini. Waziri wa mambo ya nje Sergey Lavrov alikuwa Johannesburg kuiwakilisha Russia.

Robertinho awatuliza mashabiki Simba SC
Watanzania wapewa ofa elimu bila malipo Urusi