Hatimaye mzizi wa fitna umekatwa alfajiri ya leo, baada ya bondia kutoka Mexico, Canelo Alvarez kufanikiwa kutetea mikanda ya ubingwa wa dunia uzito wa kati kwa kumpiga kwa alama mbabe kutoka Brooklyn, Marekani Daniel Jacobs.

Canelo ambaye alikuwa anapewa nafasi zaidi katika pambano hilo alikuwa na mashabiki wengi zaidi ndani ya ukumbi wa T-Mobile, Nevada, Las Vegas nchini Marekani, alifanikiwa kutawala pambano hilo katika raundi nyingi zaidi.

Majaji Dave Moretti, Steve Weisfeld na Glenn Feldman wa pambano hilo ambao ni jopo lililotumika pia kwenye pambano kati ya Canelo na Gennady Golovkin aka Triple G, wamempa ushindi Canelo kwa 115-113, 115-113 na 116-112.

Akizungumza baada ya pambano hilo, Canelo amesema lilikuwa pambano gumu na mpinzani wake amefanya kazi kubwa lakini amemshinda kama alivyoahidi.

Akizungumzia matakwa ya mashabiki kutaka apigane tena na Tripple G, Canelo amesema kuwa yeye alishamalizana na pambano hilo lakini kama mashabiki wanataka atapigana naye tena na anaamini atampiga.

Canelo na Tripple G walitoa sare kwenye pambano lao la kwanza ambalo lilizua mzozo wengi wakiamini Triple G alishinda, lakini pambano la pili Canelo alishinda.

Kwa upande wa Jacobs, amesema anaheshimu uamuzi wa majaji na kwamba ataenda kuangalia tena pambano hilo na kujipanga upya kwa nguvu zaidi kujiandaa na mapambano mengine.

Kim Jong Un ashuhudia majaribio ya makombora, Trump amwandikia ujumbe
Kikwete: Nilizungumza na Mengi kabla ya kifo chake, 'Ukweli tutaupata'