Baada ya kupatikana kwa suluhu baina ya viongozi wa benchi la ufundi la Chelsea dhidi ya Diego Costa, mshambuliaji huyo amaibuka tena na kutikisa kibiriti cha kutaka alipwe mshahara mkubwa.

Costa aliingia matatani mwishoni mwa juma lililopita baada ya kubwatukiana na meneja wa Chelsea Antonio Conte, kufuatia sakata la kutaka kuihama klabu hiyo na kutimkia Tianjin Quanjian nchini China, ametoa sharti hilo kwa viongozi wa The Blues endapo wanahitaji aendelee kubaki Stamford Bridge.

Gazeti la The Sun limeeleza kuwa, mshambuliaji huyo mzaliwa wa nchini Brazil, ameutaka uongozi wa The Blues kumlipa mshahara wa pauni 300,000 kwa juma, ambao utakaribiana na ule ambao angelipwa kama angejiunga na klabu ya Tianjin Quanjian.

Taarifa za gazeti hilo zimeongeza kuwa, Costa amefikia hatua ya kutoa sharti hilo, kutokana na mchakato wa mazungumzo ya kusaini mkataba mpya ambao unaendelea kati yake na viongozi wa Chelsea tangu mwezi Novemba mwaka 2016.

Mkataba wa sasa, unamuwezesha costa kulipwa mshahara wa pauni 150,000 kwa juma na tetesi zinaeleza kuwa huenda akazidishiwa kiasi hicho na kufikia Pauni 225,000 kwa juma.

Mkataba unaoandaliwa na Chelsea kwa ajili ya mshambuliaji huyo aliyechukua uraia wa nchini Hispania ni wa miaka mitano.

Guangzhou Evergrande Wamtengea Mshahara Mnono Arda Turan
Memphis Depay Kufanyiwa Vipimo Vya Afya