Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula ametaka elimu ya kuwatahadharisha wananchi kuhusu kujiepusha na vishawishi visivyo na tija vinavyosababisha ugawaji maeneo ya ardhi kwa ajili ya uwekezaj kwa kupewa ahadi zisizotekelezeka.

Dkt Mabula amesema hayo wakati akifungua Kikao Kazi cha Wadau wa Uandaaji, Usimamizi na Utekelezaji wa Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi nchini kilichofanyika jijini Dodoma.

‘’Tunategemea ninyi wadau mnakuwa sehemu ya kuelimisha wananchi kutambua thamani ya ardhi na kutokuwa wepesi kuachia ardhi kwa sababu ya tamaa ya wawekezaji, wanakuja halafu wanakuwa ahadi isiyotekelezeka na mwisho wa siku wananchi wanapeleka kilio serikalini’’ amesemaDkt. Mabula

Kwa mujibu wa Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, elimu itakayotolewa itakuwa ni kwa ajili ya kuwafungua akili wananchi hasa wale wa vijijini kutouwa na wasiwasi na tamaa ya kupokea vishawishi ambavyo mwisho wa siku havitekelezi.

‘’Kuna maeneo watu wa Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi wamepanga na muwekezaji anaahidi kitu ambacho hakitekelezeki  na wananchi wanakuwa na tamaa kuwa watajengewa shule, zahananti au kuchimbiwa kisima na mwekezaji ataanza mchakato kidogo kidgo lakini mwisho wa siku hakuna kinachofanyika na wakati huo ardhi ishachukuliwa na migogoro inakuwa mingi hivyo tusingependa  haya yajirudie’’

Ameitaka Tume ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi nchini kwa kushirikiana na wadau kuongeza kasi ya uelimishaji wananchi kuhusu uandaaji na utekelezaji mipango ya matumizi ardhi ili mipango hiyo inapoidhinishwa na mamlaka husika basi iweze kutekelezwa na kusimamiwa kwa umakini.

Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Allan Kijazi aliwataka washiriki wa kikao hicho cha wadau wa uandaaji, usimamizi na utekelezaji wa mipango ya matumizi ya ardhi kuja na mikakati itakayoishauri Tume ya Matumizi ya Ardhi namna bora itakayosaidia uwepo wa vipaumbele katika kuchagua maeneo ya kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi.

‘’Tanzania tunavyo vijiji visivyopungua 14,000 na kati ya hivyo takriban vijiji 2000 ndivyo vyenye mipango ya matumizi bora ya ardhi hivyo bado tunayo kazi kubwa ya kufanya ili kuongeza kasi na lazima kujiuliza tunaanzia wapi’’. Amesema Dkt Kijazi

Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Makazi Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Deogratius Kalimenze aliwataka wadau kuhakikisha kazi wanazozifanya na kukamilisha kwenye mamlaka ya serikali za mitaa taarifa zake zinawasilishwa  kwa wakati ili kufanyiwa kazi na Tume na Waziri aweze kutangaza gazeti la serikali na kusisitiza kuwa mipango yote iliyokamilika lazima itangazwe kwa wakati.

Mkurugenzi wa Taasisi ya Landesa Monica Mhoja Tume itazame upya namna bora ya kuidhinisha mipango ya matumizi bora ya ardhi na kuchapishwa kwenye gazeti la serikali.

‘’Katika mipanpo mingi ni michache tu iliyoweza kuchapishwa na kusababisha mipango mingi ionekane kutokamilika na tunaomba mchakato huu uangaliwe upya’’ amesema Monica Mhoja.

Simba SC yakanusha kumfukuza Kocha Pablo
Senegal yamuondoa Carlos Queiroz