Baada ya kuibanjua Mwadui FC bao moja kwa sifuri mjini Shinyanga jana Jumapili (April 18), Kocha Mkuu wa Simba, Didier Gomes Da Rosa amezitahadharisha timu shiriki katika ligi hiyo ambayo kwa sasa inalekea ukingoni kwa msimu huu 2020/21.

Gomez amesema kama kuna timu ina ndoto ya kushinda taji la Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu, basi wasahau kuhusu hilo kwani kikosi chake kitafanya kila jitihada kuhakikisha wanatetea ubingwa huo mapema tu.

Simba SC imeshatwaa taji la Ligi KuuTanzania mara tatu mfululizo na msimu huu wameonekana kupata upinzani mkubwa kutoka kwa watani zao Young Africans ambao wametangaza nia ya wazi ya kumaliza utawala huo.

“Najua hakuna timu ambayo inashiriki ligi bila kuwa na malengo yao binafsi, na kuna baadhi ya wapinzani wetu ambao wamejipanga kutuvua ubingwa msimu huu.

“Lakini niwahakikishie kuwa, tumejipanga kutumia faida ya michezo yetu ya viporo kuongoza msimamo wa ligi kwa tofauti ya pointi saba, na ikiwezekana kutangaza ubingwa mapema.” Amesema kocha huyo kutoka nchini Ufaransa.

Simba SC inashika nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara ikiwa na alama 52, ikitanguliwa na Young Africans yenye alama 54 huku Azam FC inashika nafasi ya tatu ikiwa na alama 50.

Rais Samia kulihutubia Bunge kwa mara ya kwanza
Rais Samia akemea uzandiki