Mbunge wa Kawe, Askofu Josephat Gwajima amesema kuwa anamhitaji aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Halima Mdee.

Askofu Gwajima aliyegombea ubunge kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu, alimshinda Mdee aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo kwa kipindi cha miaka kumi mfululizo kwa tiketi ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo. Awali, Mdee alikuwa mbunge wa viti maalum kwa kipindi cha miaka mitano.

Akizungumza hivi karibuni katika mahojiano maaluma na Dar24 Media Bungeni, Jijini Dodoma, mbunge huyo alisema kuwa anamhitaji Mdee kutokana na uzoefu wake katika jimbo hilo na utendaji wake wa kazi. Hivyo, anaamini mchango wake utamsaidia katika kuwatumikia wananchi.

“Nafahamu siasa sio uadui, na malumbano ya kwenye majukwaa sio malumbano ya maisha. Kwahiyo, mchango wake, uzoefu wake na namna alivyokuwa anatenda, namhitaji sana,” Askofu Gwajima ameiambia Dar24 Media.

“Kuna wakati mwingine nitaenda kumuona na tutazungumza mambo ya kawaida ya wananchi wa Kawe, ameishia wapi ili na mimi nianzie…. Kwahiyo yote kwa yote mimi namhitaji na najua ana mchango wa kunisaidia huko mbele ninakokwenda. Mambo ya majukwaani yamekwisha, tufani imekwisha na sasa ni majira mapya,” ameongeza.

Bofya kuangalia video ya mahojiano kwa kina

Katika hatua nyingine, mbunge huyo amesema kuwa anaanza kutekeleza ahadi alizozitoa wakati wa kampeni akianza kwa kununua trekta litakalofanya kazi ya kuboresha miundombinu katika baadhi ya maeneo ya jimbo hilo, wakati wanasubiri nguvu kubwa zaidi kutoka Serikalini.

Hitimana Thiery aondoka Namungo FC
Morocco: Sijasaini Namungo FC