Halmashauri zote nchini zilizobainika kutumia fedha za miradi ya ujenzi wa barabara kinyume cha utaratibu kwa kubadili matumizi na kulipa miradi hewa zimetakiwa kuzirudisha fedha hizo katika Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini (TARURA) ili zikafanye kazi iliyokusudiwa.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Mfuko wa Barabara nchini (RFB), Joseph Haule, ambapo amesema hayo wakati akitoa taarifa ya ukaguzi wa kiufundi na fedha kwa fedha zilizopelekwa na mfuko huo katika halmashauri mbalimbali nchini kwaajili ya ujenzi wa barabara.

“Haikubaliki yaani zaidi ya shilingi millioni 400, zitumike kinyume cha utaratibu kwa kununua madawati, kompyuta, vifaa vya ofisi, kujenga maabara za shule za sekondari na matumizi hewa kinyume na utaratibu wa matumizi ya fedha za mfuko wa barabara,” amesema Haule.

Aidha, Haule mezitaja halmashauri zinazohusika na matumizi mabaya ya fedha za barabara kuwa ni Jiji la Tanga, Manispaa ya Mtwara, Halmashauri ya Wilaya ya  Monduli, Moshi, Songea, Kilolo, Nanyumbu, Masasi na Ushetu, zingine ni halmashauri ya wilaya ya Kyerwa, Karagwe, Ngorongoro, Meru, Kondoa, Kakonko, Kalambo, na Gairo.

Kwa upande wake Meneja wa mfuko wa barabara, Eliud Nyauhenga amesema kuwa wamejipanga kuhakikisha fedha za barabara zinatumika kama ilivyokusudiwa na bodi imeongeza wataalam wa ukaguzi wa miradi inayotumia fedha za mfuko huo hivyo kuzitaka halmashauri kuongeza umakini katika utekelezaji wa miradi ya barabara.

Hata hivyo, Bodi ya Mfuko wa barabara ambayo hutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara katika halmashauri nchini imewataka wahandishi wanaosimamia fedha hizo kuongeza ufanisi ili kuwezesha fedha hizo kutekeleza miradi mingi kwa wakati na kwa kuzingatia thamani ya fedha

Ligi Kuu TZ Bara: Mechi saba kuchezwa kesho, moja jumapili
Sami Khedira, Mesut Ozil watemwa timu ya taifa