Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imetangaza mwongozo wa utoaji mikopo kwa mwaka wa masomo 2019/2020 unaotaja sifa, vigezo na utaratibu wa kuwasilisha maombi ya mikopo ya elimu ya juu.

Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB Abdul-Razaq Badru amewaambia wanahabari jijini Dar es salaam kuwa lengo la kutoa mwongozo huo ni kuwawezesha waombaji mikopo kuandaa nyaraka muhimu zinazotakiwa.

Kwa mujibu wa Badru, amesema mfumo wa maombi kwa njia ya mtandao utafunguliwa Juni 15, 2019 na utafungwa Agosti 15, 2019.

“Uzoefu wetu unaonyesha kuwa waombaji wengi hukimbilia kwenye mtandao na kujaza fomu za maombi wakati mwingine bila kusoma mwongozo. Mwaka huu tumetoa mwongozo huu kwanza ili wausome kwa wiki takribani mbili kabla ya kuruhusiwa kuanza kujaza fomu kwa njia ya mtandao,” amesema Badru na kuongeza kuwa katika mwaka 2018/2019, waombaji zaidi ya 9,000 kati ya 57,539 waliokuwa na sifa za msingi walikosea kujaza fomu za maombi.

Ili kutatua tatizo hilo mwaka 2019/2020, Badru amesema HESLB imetembelea shule za sekondari 81 katika mikoa 17 ya Tanzania Bara na Zanzibar na kukutana na wanafunzi 27,489 ambao walielimishwa kuhusu sifa na utaratibu wa kuomba mkopo kwa usahihi.

Mkurugenzi Mtendaji huyo amesema mwongozo huo unapatikana katika lugha za kiingereza na kiswahili katika tovuti ya HESLB ambayo ni www.heslb.go.tz.

“Pamoja na mwongozo huo, pia tumeandaa kijitabu chenye maswali na majibu yanayoelekeza namna ya kuomba mkopo kwa lugha ya kiswahili … nacho pia kinapatikana kwenye tovuti yetu na tunawashauri wakisome,” amesema Mkurugenzi Mtendaji huyo.

Aidha amesema waombaji wote wanatakiwa kuandaa nyaraka muhimu kama vile vyeti vya kuzaliwa ambavyo vimethibitishwa na Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA) au Wakala wa Usajili wa Matukio ya Kijamii Zanzibar (ZCSRA) na kwa waombaji mikopo ambao wazazi wao wamefariki dunia, watatakiwa kuwa na nakala za vyeti vya vifo ambavyo vimethibitishwa na RITA au ZCSRA.

“Vilevile tunafahamu kuwa kuna wanafunzi waliofadhiliwa na taasisi mbalimbali katika masomo yao ya sekondari au stashahada, hawa wanatakiwa kuwa na barua kutoka katika taasisi hizo,” amesema Badru katika mkutano huo uliohudhuriwa na Mkurugenzi wa Upangaji Mikopo wa HESLB Dkt. Veronika Nyahende.

Kwa wanafunzi wenye ulemavu au wenye wazazi wenye ulemavu, Badru amesema wanapaswa kuwa na barua zinazothibitisha ulemavu wao kutoka kwa waganga wakuu wa wilaya au mikoa.

Maeneo muhimu yaliyoboreshwa kwa 2019/2020

Katika mkutano huo, Mkurugenzi Mtendaji huyo aligusia maeneo muhimu yaliyoboreshwa katika utoaji mikopo kwa lengo la kuwafikia wanafunzi wahitaji wengi zaidi.

“Baada ya kupokea maoni ya wadau, tumeongeza umri wa waombaji mikopo kutoka miaka 33 hadi 35 na pia mwaka huu tutapokea maombi kwa wanafunzi waliomaliza kidato cha sita au stashahada ndani ya miaka mitano iliyopita … kabla ilikuwa miaka mitatu tu,” amesema Badru.

Malengo na bajeti

Katika mwaka wa masomo 2019/2020, Serikali kupitia HESLB imepanga kutoa mikopo na ruzuku ya elimu ya juu yenye thamani ya TZS 450 bilioni kwa jumla ya wanafunzi 128,285. Kati ya hao, wanafunzi 45,000 watakuwa wa mwaka wa kwanza. Mwaka huu 2018/2019, unaoelekea mwisho; jumla ya TZS 427.5 bilioni zilitolewa kwa jumla ya wanafunzi 123,000.

Dawati la huduma kwa wateja

Pamoja na mwongozo uliotolewa, dawati la huduma kwa wateja litakuwa wazi ili kutoa ufafanuzi pale utakapohitajika. Wateja wetu pia wanaweza kupiga simu au kutuandikia barua pepe anuani na namba: Simu: 0736 665533 au 0738 66 55 33 au 022 5507910; Barua pepe: adcp@heslb.go.tz au info@heslb.go.tz

Video: Wanaume wa Kinondoni wafunguka tatizo la nguvu za kiume, balaa
TRA yatangaza adhabu kali kwa wasiodai wala kutoa risiti