Uwanja wa Taifa umekuwa kwenye matengenezo ya sehemu ya kuchezea (Pitch) kwa takribani mwezi mmoja sasa,  mara ya mwisho uwanja huo ulitumika kwenye mchezo wa Ngao ya jamii uliozikutanisha Simba na Yanga Agosti 23 mwaka huu na kesho yake nyasi za uwanja huo zilifumuliwa na kuanza matengenezo rasmi.

Hii ni hawamu ya pili ya matengenezo baada ya awali uwanja huo kufanyiwa matengenezo kabla ya ujio wa klabu ya Everton mwezi juni ambapo kampuni ya SportPesa iliingia gharama za kukarabati sehemu ya kuchezea ikiwemo kuweka nyasi mpya, vyumba vya kubadilishia nguo pamoja na vyoo.

Abbas Tarimba ambaye ni Mkurugenzi wa utawala na utekelezaji wa SportPesa ametoa ufafanuzi juu ya sababu za  matengenezo akisema kuwa sababu kubwa ya SportPesa kurekebisha uwanja huo haikuwa tu kwa sababu ya ujio wa  Everton bali ni kutoa mchango kwa Tanzania ili kuweza kuwa na miundombinu bora zaidi ambayo ina viwango vya kimataifa.

SportPesa ambayo ni kampuni ya michezo ya kubashiri imeendelea na ukarabati wa uwanja wa taifa kwa hawamu ya pili huku serikali kupitia  Mkurugenzi wa michezo wa Wizara ya Habari, Sanaa, utamaduni na michezo Mh. Yusuph Singo ikiipongeza kampuni hiyo.

”SportPesa kwa kweli wameonesha mfano, wamejitahidi kudhamini vilabu mbalimbali, wametusaidia kurekebisha uwanja na kama sikosei gharama za kurekebisha uwanja zimefika takribani bilioni 1.3, ni hela nyingi sana hivyo sisi tunawashukuru sana” alisema Yusuph Singo.

 

Benjamin Mendy Kutibiwa Barcelona
Saudi Arabia yaruhusu wanawake kuendesha magari