Naibu Waziri wa Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhandisi Maryprisca Mahundi amepongeza uwepo kwa huduma bora za mawasiliano ya simu na intaneti katika eneo la forodha lililopo katika mpaka wa Tunduma.
Naibu Waziri Mahundi alitoa pongezi hizo wakati wa ziara yake ya kukagua upatikanaji wa huduma za mawasiliano maeneo ya mipakani, katika mpaka wa Tunduma mkoani Songwe.
Amesema, “Mawasiliano katika mpaka huu wa Tanzania na Zambia yameboreshwa sana, na tunashukuru Mhe. Rais Samia kwa nia yake ya kuipeleka Tanzania kidijitali. Hapa, huduma za simu na intaneti zimeimarishwa.”
Mahundi alitumia fursa hiyo kuisisitiza kampuni ya Airtel Tanzania kukamilisha ujenzi wa mnara wa mawasiliano ya simu kupitia Mradi wa Tanzania Kidijitali katika Wilaya ya Momba, hasa katika Kata ya Nzoka, Kijiji cha Namtambala, ili kuboresha huduma za Mawasiliano katika eneo husika.
“Nyote mnafahamu umuhimu wa huduma za mawasiliano. Tunahitaji kuona wananchi wakifurahia elimu na taarifa mbalimbali zinazotolewa kupitia vyombo kama vile redio na simu,” alibainisha Mahundi.
Akitoa salamu, Mkuu wa Wilaya ya Momba, Elias Mwandobo aliipongeza Wizara kwa juhudi zake katika kuboresha huduma za mawasiliano, pamoja na kutoa rai kwa wananchi kutumia huduma hizi ili kujipatia maendeleo, ikiwemo sekta ya kilimo.
Naye Meneja Msaidizi wa Idara ya Forodha Mkoa wa Songwe, Nsajigwa Mwambegele ameishukuru serikali kupitia Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kwa kuwezesha huduma bora katika eneo hilo.