Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR – TAMISEMI), Selemani Jafo amwewasilisha Muswada wa Sheria ya Kulitangaza Jiji la Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi katika mkutano wa kumi na mbili wa kikao cha kwanza cha Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Jafo amesema kuwa dhumuni la muswada huo ni kupendekeza kutungwa kwa sheria ambayo italitangaza rasmi Jiji la Dodoma kuwa makao makuu ya nchi na makao makuu ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Amesema kuwa chimbuko la hoja ya kutunga sheria hiyo ni kukosekana kwa sheria inayotambua na kuweka misingi ya uendelezaji wa makao makuu ya nchi, hivyo hatua ya kulitambua jiji la Dodoma kama makao makuu ya nchi itachochea ukuaji wa mji huo na maeneo yanayozunguka mkoa huo kiuchumi na kijamii.

“Kukosekana kwa sheria inayotambua Dodoma kuwa makao makuu ya nchi kulisababisha uendelezaji wa makao makuu ya nchi kutofikia malengo, hivyo msingi wa kutunga sheria hii ni kutambua kisheria jiji la Dodoma kuwa makao makuu ya nchi” amesema Waziri Jafo.

Akifafanua kuhusu muswada aliowasilisha mbele ya Spika, Job Ndugai, Jafo amesema muswada huo utakuwa na vifungu sita vikiwemo vya utangulizi, matumizi, tafsiri ya maneno yaliyotumika, kulitangaza  Jiji la Dodoma kama makao makuu ya nchi na mwisho ni kifungu ambacho kimeweka masharti ya kubadilisha makao makuu ya nchi.

Uamuzi wa kuwasilisha muswada wa kulitanganza jiji la Dodoma kuwa makao makuu ya nchi na serikali, ni mwendelezo wa hatua za kimageuzi zinazofanywa na Serikali ya awamu ya Tano chini ya Rais Dkt. John Pombe  Joseph  Magufuli.

Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Septemba 5, 2018
Walizibinya Kende zangu na kunipiga mabuti- Bobi Wine