Beki wa kati wa mabingwa wa soka nchini Italia Juventus FC Giorgio Chiellini, amejumuishwa kwenye kikosi kilichowasilishwa kwenye shirikisho la soka barani Ulaya UEFA, kwa ajili ya michezo ya hatua ya 16 bora ya ligi ya mabingwa (UEFA Champions League).

Chiellini, mwenye umri wa miaka 35, amecheza mchezo mmoja msimu huu, na amekua nje ya uwanja baada ya kufanyiwa upasuaji wa goti, mapema mwezi Septemba mwaka jana (2019).

Beki huyo ambaye pia ni nahodha wa Juventus, anatarajiwa kurejea uwanjani kati ya mwezi huu ama mwezi ujao, hatua ambayo imelisukuma benchi la ufundi linalooongozwa na Maurizio Sarri kumjumuisha kwenye kikosi kilichowasilishwa UEFA.

Kanuni za michuano ya ligi ya mabingwa barani Ulaya (UEFA Champions League) huzitaka klabu shiriki kuwasilisha majina ya wachezaji 22, ambao watashiriki kwenye hatua ya 16 bora na kuendelea, hasa baada ya kipindi cha dirisha dogo la usajili kufungwa mwezi Januari kila mwaka.

Juventus FC watapamban na Olympic Lyon kwenye hatua ya 16 bora, na mchezo wa kwanza watakua ugenini nchini Ufaransa Februari 26, kabla ya kurejea mjini Turin, Italia kwa mchezo wa mkondo wa pili ambao utaunguruma Machi 17.

Kikosi cha Juventus FC kilichowasilishwa UEFA kwa ajili ya hatua ya 16 bora ya ligi ya mabingwa barani Ulaya (UEFA Champions League): Gianluigi Buffon, Carlo Pinsoglio, Wojciech Szczesny; Leonardo Bonucci, Giorgio Chiellini, Danilo na  Matthijs de Ligt.

Wengine ni Mattia De Sciglio, Daniele Rugani, Alex Sandro; Rodrigo Bentancur, Juan Cuadrado, Sami Khedira, Blaise Matuidi, Miralem Pjanic, Adrien Rabiot, Aaron Ramsey; Federico Bernardeschi, Douglas Costa, Paulo Dybala, Gonzalo Higuain na Cristiano Ronaldo.

Mvutano waibuka Bungeni sheria ya wabakaji kuhasiwa
Magufuli amkumbuka Moi kwa kufufua Jumuiya ya Afrika Mashariki