Mgombea urais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania kupitia chama cha mapinduzi CCM Dkt John Pombe Magufuli  amewataka wananchi kuwachagua viongozi wenye uwezo wa kujenga hoja badala ya kuchagua watu waliosoma sana.

Dokta Magufuli ameyazungumza hayo leo Septemba 28, akiwahutubia wananchi wa Mlowa ambako Mgombea Ubunge wa CCM ni Livingstone Lusinde, wakati akiwa njiani kuelekea Iringa.

 “Nileteeni wa CCM ambao ninao uwezo wa kuwatumbua mkinileta mwingne sina uwezo wa kumtumiua pesa zitaliwa na sina cha kumfanya, Mbunge wenu Lusinde ni mchapakazi, narudia Ubunge sio Madegree ni uwezo wa kujenga hoja,” amesema Magufuli.

Aidha rais Magufuli amemtaka mkuu wa mkoa wa Dodoma dokta Binilith Satano Mahenge kumuagiza meneja wa TANROADS Mkoa wa Dodoma ndani ya miezi miwili Barabara ya Mlowa kwenda Mvumi itangazwe tenda kwa ajili ya kujengwa kwa kiwango cha lami ili kurahisisha usafiri wa wagonjwa wanaopelekwa Mvumi .

JPM amejinadi kuwa anataka kulifanya jimbo hilo ambalo lipo karibu na Makao makuu ya nchi liwe “lenye kunusanusa makao makuu”.

“Hata kuhamia Dodoma haikuwa rahisi tumekaa zaidi ya miaka 47 hilo halijawezekana ila sisi tumeweza, tunajenga uwanja wa Ndege mkubwa Msalato, ndege zote za kimataifa zitakuwa zinatua hapa, tumejenga Reli ya kisasa, Soko la kisasa, Stendi ya kisasa, tunataka kutimiza ndoto ya Baba wa Taifa,” amesema Magufuli.

Google yapiga panga App 17
Sven Vandenbroeck: Nimeridhishwa na kiwango