Mshambuliaji wa Liverpool Sadio Mane ameendelea kujitetea, licha ya rufaa yake ya kupinga kadi nyekundu aliyoonyeshwa mwishoni mwa juma lililopita dhidi ya Man City kuwekwa kapuni na chama cha soka nchini England (FA).

Mane amesema bado anashindwa kueleweka na jamii ya wanasoka nchini England na duniani kwa ujumla, kwa kosa alilolifanya dhidi ya mlinda mlango wa Man City Ederson kwa kumpiga teke la uso.

Mshambuliaji huyo kutoka nchini Senegal amesema hatochoka kujitetea kwa dhana potovu zinazoendelea kuchukua nafasi dhidi yake, lakini ukweli ni kwamba hakuwa na kusudio la kumuumiza kipa huyo ambaye alishindwa kuendelea na mchezo.

“Mwamuzi aliona kuna ulazima wa mimi kuadhibiwa kwa kadi nyekundu, lakini halimaanishi ipo haja ya kuhalalisha adhabu hiyo kwa kunituhumu kufanya kosa kwa makusudi, ninataka nieleweke sikufanya vile kwa kukusudia, ilikua bahati mbaya ambayo inaweza kumtokea yoyote anapokua uwanjani.

“Ninajitahidi kufikisha ujumbe huu kwa kila mdau anaenilaumu kwa kosa lile, ninaomba nieleweke, na sitochoka kujitetea.

“Ilikua ni sehemu ya kuwania mpira kati yangu na Ederson, ukifuatilia katika picha za video utaona tukio hilo vizuri, kwa hiyo sipendi kuona watu wakinilamu wakati yapo makosa mengine yaliwahi kufanyika na yalifumbiwa macho, zaidi ya hili nililofanya ambalo kwangu halikua la makusudi.” Amesema Mane

Hata hivyo Mane ameahidi kubadilika endapo itatokea anakutana na tukio kama hilo: “Ninafikiri umefikia wakati wa kuangalia namna ya kuumiliki mpira kabla haujamkaribia mpinzani wangu, najua itawezekana. Aliongeza Mane

Mane atakosa mchezo dhidi ya Burnley utakaochezwa mwishoni mwa juma hili. Pia atakosa michezo miwili ya kombe la ligi na ligi ya England dhidi ya Leicester City.

Kendrick, Dj Khaled watajwa zaidi tuzo za BET
Rekodi ya Azam FC, Kagera Sugar ligi kuu Tanzania bara