Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Constantine Kanyasu ameiagiza Halmashauri ya wilaya Buchosa mkoani Mwanza kupitia upya ramani ya vijiji vilivyopo ndani ya hifadhi ya msitu wa Kisiwa cha Maisome kwa ajili ya kutatua mgogoro wa ardhi uliopo kati ya wanavijiji na Halmashauri hiyo.

Ametoa agizo alipokuwa wilayani humo kwa ziara ya siku mbili ya kutatua kero za wananchi mara baada ya kusikiliza malalamiko kutoka kwa wananchi wa kijiji cha Kisaba na Busikimbi wakati wa mkutano wa hadhara uliofanyika katika kijiji cha Kisaba wakidai kuwa TFS imechukua baadhi ya maeneo ya vijiji hivyo.

Aidha, ameuagiza Uongozi wa Halmashauri hiyo ushirikiane na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS)  wakati wa inapofanya upya mapitio ya ramani hiyo ili kuweza kumaliza tatizo la mgogoro huo uliopo kufuatia baadhi ya maeneo ya wananchi kuingia ndani ya Hifadhi ya msitu huo kwa mujibu ramani iliyopo.

Katika vijiji hivyo jumla ya ekari 103 za wananchi walizokuwa wakizitumia katika shughuli za kiuchumi zinadaiwa kuingia ndani ya Hifadhi ya msitu iliyo chini ya TFS

”Wachora ramani sio TFS, hivyo TFS wanatumia ramani iliyokwisha tengenezwa na halmashauri hiyo kutokana na hilo wanatakiwa kupitia upya na kuondoa mgogoro,”amesema Kanyasu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa halmashauri ya Buchosa, Crispin Luanda amesema kuwa maagizo hayo atayatekeleza kwa wakati ili kufanikisha suala hilo .

Naye Mbunge wa jimbo la Buchosa Dkt. Charles Tizeba amemshukuru Naibu wa Waziri huyo kwa kutatua mgogoro huo ambao ulikuwa kero kwa wananchi.

Solskjaer awapa mtihani Sanchez na Lukaku, ‘kazi ni kwao’
Magaidi wateka mji, wasali pamoja na raia