Mwanamuziki wa kufoka foka Kanye West amekubali kutunza watoto wake wanne kwa ushirikiano na mke wake wa zamani Kim Kardashian.

Hatua yake inafuatia ombi la talaka lililowasilishwa na Kardashian tarehe 19 Februari, ambalo lilianzisha mchakato wa kumaliza ndoa yao ambayo imedumu kwa takriban miaka saba.

Katika maombi yao wasanii hao wawili nyota na waliokuwa wanandoa, wamekubaliana kutengana kufuatia tofauti ambazo haziwezi kusuluhishwa.

Kim na Kanye wamekubaliana kwamba hakuna kati yao anayehitaji msaada wa mwenzake.

Kwa mujibu wa ombi la Kardashian, walitenganisha mali zao wakati wote wa ndoa yao kutokana na makubaliano yaliofikiwa kabla ya kuoana.

West na Kardashian wana mabinti wawili – North na Chicago, walio na umri wa miaka saba na mitatu, na wavulana wawili Saint mwenye umri wa miaka mitano na Psalm ambaye ana umri wa mwezi mmoja pekee.

Wanandoa hao ni miongoni mwa mastaa maarufu zaidi duniani, wote wakipata ufuasi mkubwa kivyao na ndoa yao imekuwa mojawapo ya zinazofuatiliwa kwa karibu katika miongo ya hivi karibuni.

Kardashian, 40, alipata umaarufu mwaka 2007 kama nyota kipindi cha uhalisia cha televisheni kuhusu familia yake, Keeping Up With The Kardashians.

West, 43, ni mmoja wa watu wenye majina tajika katika ulimwengu wa muziki wa rap, na anatambuliwa kutokana na vibao kama vile Stronger, Jesus Walks na Gold Digger. Pia amepata ufanisi kama mwanamitindo wa nguo.

Hasira za kizungu!: Mwandishi wa habari avunjavunja simu baada ya kumzingua akiendelea na semina mtandaoni
Tanzania daima wazungumza na Waziri Bashungwa