Kocha Mkuu wa Young Africans Cedrick Kaze amewaita mashabiki wa klabu hiyo Uwanja wa Benjamin Mkapa, kwa ajili ya kuishangilia timu yao, kwenye mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya JKT Tanzania Kesho Jumamosi, Novemba 28.

Mchezo huo uliokua umepangwa kuanza mishale ya saa moja usiku, umerudishwa nyuma, na utachezwa kuanzia saa kumi jioni.

Kocha Kaze amesema mashabiki wanapaswa kufika uwanjani kuendelea kuishangilia timu yao, ili kuendelea kufanikisha malengo waliyojiwekea msimu huu.

“Lengo letu ni kuhakikisha tunaendelea kufanya vizuri, na mwishoni mwa msimu huu tuweze kutwaa ubingwa, hili halitowezekana kama mashabiki hawatokua tayari kushirikiana na timu yao kwa kufika uwanjani.”

“Tunaomba mjitokeze kwa wingi kutuunga mkono kwenye mchezo unaofuata dhidi ya JKT Tanzania. Furaha yenu ndio heshima yetu”. Amesema Kaze.

Katika hatua nyingine kocha huyo kutoka nchini Burundi, amewapongeza mashabiki kwa kuiunga mkono timu yao katika mchezo uliopita dhidi ya Azam FC, ulimalizika kwa ushindi wa bao moja kwa sifuri lililofungwa na Deus Kaseke, Uwanja wa Azam Complex Chamazi, Dar es salaam.

“Ushindi dhidi ya Azam FC ni wenu Wananchi popote mlipo. Tunaendelea kupambana ili kurudisha heshima kwenu na kwa sisi wote,” amesema Kaze.

Young Africans inaongoza msimamo wa Ligi Kuu kwa kufikisha alama 28, ikifuatiwa na Azam FC wenye alama 25,huku mabingwa watetezi Simba SC wakishika nafasi ya tatu kwakuwana alama 23.

NEC yawajibu CHADEMA
Rage awaibia siri Simba SC