Klabu ya Simba imetangaza rasmi kuwa wachezaji wake wawili Aubin Kramo na Henock Inonga waliokuwa majeruhi, wameanza mazoezi kwa ajili ya maandalizi ya mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika hatua ya raundi ya kwanza dhidi ya Power Dynamos ya Zambia.

Meneja Habari na Mawasiliano wa Klabu hiyo, Ahmed Ally, amesema wachezaji hao walianza mazoezi juzi kwenye Uwanja wa Mo Arena, Bunju, baada ya kuwa nje kwa zaidi ya wiki mbili wakiwa majeruhi.

“Kikosi kilianza mazoezi juzi Jumanne, wachezaji wetu wote wamerejea kambini na bahati nzuri hakuna mchezaji ambaye alisafiri nje ya nchi na taarifa njema ambayo wanachama na mashabiki wa Simba SC wanapaswa kuifurahia ni kwamba Aubin Kramo ameanza mazoezi.

“Kumbuka alipewa wiki moja ya mapumziko, amefanya mazoezi juzi jumanne jioni  akiwa yupo fiti kabisa, vile vile beki wetu wa kati Henock Inonga naye amerejea, yeye alipewa muda mrefu kidogo wa kupumzika ila kwa sasa yuko timamu na amefanya mazoezi na wenzake, kikubwa tuko tayari kuelekea kwenye mchezo wetu wa Raundi ya Kwanza Ligi ya Mabingwa dhidi ya Power Dynamos,” amesema Ahmed.

Inonga aliumia katika mechi ya nusu fainali ya Ngao ya Jamii dhidi ya Singida Fountain Gate Agosti 10 na Kramo aliumia mazoezini kabla ya michezo ya Ngao ya Jamii.

Klabu hiyo pia imesema itacheza mechi moja au zaidi za kirafiki kwa ajili ya kuwaweka fiti wachezaji wake kutokana na kukaa muda mrefu bila kucheza.

“Kwa mujibu wa kocha wetu ni lazima tupate mechi za kirafiki, mara ya mwisho tulicheza dhidi ya Dodoma Jiji, tumekaa muda kidogo na kuna wiki nyingine za kukaa bila michezo kwa hiyo lazima tucheze mechi za kirafiki ili kunyanyua utimamu wa mwili na pumzi za wachezaji,” amesema Ahmed.

Aidha, amesema kuwa klabu hiyo imepata barua rasmni kutoka Shirikisho la Soka Barani Afrika (CAF) kuwa mechi yao itachezwa Jumamosi ya Septemba 16 Uwanja wa Levy Mwanawasa Ndola, Zambia.

Cesc Fabregas azichambua Arsenal, Chelsea
Al Merrikh kujitafuta kwa Rayon Sports