Meneja wa muda wa Klabu ya Chelsea Frank Lampard ameowamba mashabiki wa klabu hiyo kuwasapoti Raheem Sterling na Hakim Ziyech baada ya mastaa hao kuzomewa wakati wakiingia uwanjani katika mchezo wa mwishoni mwa juma lililopita, ambao walishinda mabao 3-1 dhidi ya Bournemouth.

Mashabiki wa Chelsea pia walimtolea maneno makali mmiliki wa sasa, Todd Boehly huku wakiimba kwa kutaja jina la Roman Abramovich.

Licha ya Sterling na Ziyech kuzomewa waling’aa katika mechi hiyo wakiwatengenezea nafasi za kufunga Benoit Badiashile na Joao Felix kwenye mchezo huo wa Ligi Kuu England.

Chelsea ilipata ushindi kwenye ligi kwa mara ya kwanza na kuhitimisha msururu wa vichapo sita mfululizo na kuweka rekodi ya mwendo mbovu zaidi katika historia ya Chelsea.

Akizungumza baada ya mchezo huo Lampard amesema kwa sasa umoja unahitajika kati ya mashabiki na wachezaji kwani ndio njia imara ya kurudisha matumaini kwenye timu.

“Mashabiki wetu walikuwa na shangwe, tunawashukuru kwa sapoti yao, nilizungumza na wachezaji baada ya mechi na kila mtu alijisikia vizuri, sizungumzii kilichowatokea Ziyech na Sterling, hii ni klabu kubwa, mashabiki wanataka mafanikio kwa sababu ndio nembo ya klabu, nadhani tukiungana katika kipindi hiki naamini mambo yatakuwa mazuri tu.” amesema

Jamie Carragher ampigia saluti Mo Salah
Wananchi msijenge mabondeni ni hatari - Serikali