Mwanasheria mkuu wa Chadema ambaye pia ni mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu ametofautisha kilichomkuta Edward Lowassa kwenye sakata la Richmond na kilichomkuta Profesa Sospeter Muhongo kwenye sakata la Escrow bungeni.

Akiongea katika kipindi cha Mada moto cha Channel Ten, Lissu alieleza kuwa kwa kutumia ripoti za kamati za bunge zilizomhukumu Lowassa mwaka 2008 na ripoti za kamati ya bunge ilizomhukumu Profesa Muhongo mwaka 2014/2015 kuna utofauti mkubwa.

Alisema kuwa ripoti ya Mwakyembe ilieleza kuwa Lowassa anawajibika kwa makosa ya watu watano wa chini yake ambao aliwataja majina na kwamba hakuna sehemu ilimtaja Lowassa kuhusika moja kwa moja na sakata la Richmond.

Alisema kuwa kamati Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) iliyokuwa chini ya Zitto Kabwe na Deo Filikunjombe, ilieleza wazi kuwa Profesa Muhongo alishiriki kudanganya kuwa fedha zile hazikuwa za umma na baadaye ikabainishwa na kamati hiyo kuwa zilikuwa fedha za umma.

“Kwa mujibu wa kamati ya Mwakyembe, Lowassa aliwajibika kwa sababu ya makosa ya hawa watu… Sasa hayo ni ya Lowassa. Yanalingana kiasi gani na ya Profesa Muhongo, yanalingana kiasi gani na ya Profesa Muhongo aliyesema kuwa bilioni 300 na ushee zilizotolewa Benki Kuu zikagawanywa kama njugu ni hela binafsi.

“CAG akachunguza akasema kuna hela za Umma, Takukuru wakachunguza hawajatuletea taarifa bungeni mpaka leo. Bunge likachunguza likasema hizi ni fedha za umma na hawa watu wawajibike na wakawajibishwa. Kuna ulingano gani hapo? Na hapo nazungumzia taarifa za kamati hizi mbili za bunge,” alisema Lissu.

Alikosoa uteuzi wa Profesa Muhongo akidai kuwa Bunge liliazimia kumfukuza na leo serikali inamrudisha kama vile hakuna kilichotokea hata kabla mwaka mmoja haujapita.

Picha: Bilionea Wa Unga 'El Chapo' aliyetoroka Gerezani Akamatwa tena
Serikali yalegeza masharti Bomoabomoa, Yamtimua Mwanasheria aliyemuokoa Lwakatare