Saa kadhaa zikisalia kabla ya kuanza kwa hafla ya kutangazwa kwa Mchezaji Bora wa Dunia wa FIFA, kiungo na nahodha wa timu ya taifa ya Croatia Luka Modric, anapewa nafasi kubwa ya kuwabwaga wapinzani wake Mohamed Salah na Cristiano Ronaldo.

Hafla ya kutangazwa kwa mshindi wa tuzo hilo kwa mwaka 2017/18 inatarajiwa kufanyika baadaye hii leo jijini London nchini Uingereza na kuhudhuria na watu mbalimbali kutoka kila pande ya dunia.

Baadhi ya vyombo vya habari vimeonyesha kumpa nafasi Modric tofauti na wapinzani wake, kwa kuamini makubwa na ushirikiano aliouonyesha akiwa na klabu ya Real Madrid na timu yake ya taifa, yatakua chachu ya kutajwa kama mshindi wa tuzo ya mchezaji bora wa dunia wa FIFA.

Tayari kura zimeshapigwa na mpaka sasa haifahamiki nani atatangazwa kuwa mshindi, lakini inaaminika vigezo vilivyotumika kumpa Modric tuzo ya mchezaji bora wa barani Ulaya na mchezaji bora wa fainali za kombe la dunia, ndivyo vitakavyombeba usiku wa leo.

Wakati Modric akipewa nafasi kubwa ya kutangazwa kuwa mchezaji bora wa dunia, kocha mkuu wa timu ya taifa ya Ufaransa Didier Deschamps, naye anapewa nafasi ya kutangazwa kuwa kocha bora wa dunia wa FIFA, kwa kuwashinda wapinzani wake Zinedine Zidane aliyekuwa Real Madrid na Zlatko Dalic (Kocha wa timu ya taifa ya Croatia).

Hata hivyo mpaka sasa mvutano unaendelea katika tuzo ya mlinda mlango bora inayowaniwa na Thibaut Courtois, Kasper Schmeichel na Hugo Lloris.

Katika kipengele hicho vyombo vya habari vilivyojikita kutabiri nani ataibuka mshindi usiku wa leo, vimeshindwa kutia neno lolote, na badala yake wameacha na kusubiri ili kuona nani ataibuka kidedea.

Pia tuzo ya mchezaji bora wa kike wa FIFA inayowaniwa na Lyon duo Ada Hegerberg, Dzsenifer Marozsan na  Marta, bado ni kuzungumkuti.

Hali kadhalika tuzo ya goli bora la mwaka inayowahusisha wachezaji Gareth Bale, Lionel Messi, Cristiano Ronaldo, Mohamed Salah, Benjamin Pavard, Ricardo Quaresma, Denis Cheryshev, Lazaros Christodoupoulos, Giorgian de Arrascaeta  na Riley McGee nayo imezua mjadala.

Lakini badhi ya vyombo vya habari vinahisi huenda tuzo hiyo ikaenda kwa mshambuliaji wa FC Barcelona na Argentina Lionel Messi, kufuatia bao lake alilolifunga dhidi ya Nigeria wakati wa fainali za kombe la dunia 2018.

Bao la ugenini lapelekwa mkutano mkuu UEFA
Video: Tunapata tabu sana kuwavumilia Chadema- Polepole