Mahakama huko Pennsylvania Marekani imepangua kesi iliyokua imefunguliwa na upande wa Rais Donald Trump kupinga matokeo ya uchaguzi ambapo walikua wakitaka kura zilizopigwa kwa njia ya posta ziondolewe kwenye hesabu.

Hakimu Matthew Brann, amesema hakuona chochote cha msingi kwenye kesi hiyo ambayo inahusu madai ya wizi wa kura.

Kampeni ya Trump ilisema kuwa jimbo hilo limekiuka katiba ya Marekani inayolinda pande zote kwa madai kuwa wapiga kura wa Democratic waliruhusiwa kurekebisha makosa waliyofanya katika kura zao, huku wale wa chama cha Republican wakinyimwa fursa hiyo.

Hata hivyo Jaji Brann ametupilia mbali madai hayo na kusema kuwa hata kama timu ya Trump ilikuwa inatafuta msingi wa kesi wazilowasilisha, timu hiyo ilivuka mpaka wakati wanatafuta suluhisho.

Baadhi ya wana Republican watoa wito kwa rais Trump kukubali kuwa ameshindwa lakini baada ya hakimu wa Pennsylvania kutoa uamuzi wake, Seneta wa jimbo hilo wa chama cha Republican amesema sasa Trump amemaliza njia alizokuwa nazo kupinga matokeo ya uchaguzi na kumsihi akubali matokeo.

Hata hivyo, wakili binafsi wa Trump, Rudy Giuliani, amesema katika taarifa atapinga uamuzi huo: “Uamuzi wa leo unaonekana kusaidia katika mkakati wetu wa kuwasilisha kesi yetu katika mahakama ya juu zaidi,” amesema wakili Giuliani.

Hii sio kesi ya kwanza kupanguliwa Mahakamani kuhusu madai hayo ya wizi wa kura kwa upande wa Trump, ambaye amekataa kukubali kwamba alishindwa kihalali kwenye Uchaguzi Mkuu wa Marekani uliofanyika Novemba 3 mwaka huu.

Bobi Wine kuendelea na kampeni
Prof. Kabudi : Hatutakubali Kudhalilishwa