Mahakama nchini  Rwanda imemnyima dhamana Paul Rusesabagina, aliyepata umaarufu kupitia filamu ya Hotel Rwanda, kwa kusema kuwa mashtaka ya ugaidi na mengine dhidi yake ni mazito na kuwa anapaswa kusalia kizuizini kwa siku nyingine 30.

Rusesabagina ambaye ni raia wa Ubelgiji na ana kibali cha kuishi Marekani amekuwa mkosoaji mkubwa wa Rais Paul Kagame, alishtakiwa wiki hii kwa makosa 13 ikiwemo kosa la kufadhili ugaidi, mauaji, kutumikisha watoto kijeshi na kuunda kikundi cha waasi.

Ingawa bado haijajulikana kesi yake itaanza lini, lakini iwapo atapatikana na hatia, huenda akahukumiwa kifungo cha miaka 25 gerezani.

Akiongea na gazeti la Marekani la New York Times, mbele ya maafisa wa Rwanda, Rusesabagina mwenye umri wa miaka 66, amesema alidhani kuwa ndege aliyokuwa ameabiri kutoka Dubai ilikuwa inaenda Burundi ambako alitarajiwa kuzungumza na makanisa nchini humo.

Hata hivyo, mahakama ya Rwanda imesema kuwa Rusesabagina alikamatwa katika uwanja wa kimataifa wa Kigali, taarifa ambayo ni kinyume na ile iliyotolewa na polisi kuwa alikamatwa kupitia waranti ya kimataifa.

Habari kubwa kwenye magazeti leo, Septemba 19, 2020
Miradi ya maji Busega yatumia Mabilioni