Mahakama ya Zimbabwe imeamua kumpa dhamana mfanyabiashara mdogo (machinga) aliyekamatwa kwa tuhuma za kumtukana Rais Robert Mugabe kuwa ‘ni mzee asiye hai na anayeota ndoto za mchana’.

Mahakama hiyo imemuachia mfanyabiashara huyo ambaye ni mwenyekiti wa umoja wa wafanyabiashara wadogo (wamachinga) nchini humo, Sten Zvorwadza kwa dhamana ya $200.

Zvorwadza, alishtakiwa kwa kosa la kumtukana Rais na kudharau Mamlaka halali ya Rais.

Mwenyekiti huyo wa wamachinga alikamatwa baada ya kukaririwa na vyombo vya habari akilaani amri ya Rais Mugabe ya kuwaondoa wamachinga wote kwenye mitaa ya jiji la Harare na kuwahamishia katika maeneo waliyotengewa kwa lengo la kulifanya jiji hilo kuwa safi kuliko majiji yote.

Gazeti la Daily News la Zimbabwe limemkariri Zvorwadza akieleza kuwa, “kama sekta isiyo rasmi hatutasikiliza upuuzi. Mugabe ni mzee na anaota ndoto za mchana.”

“Mugabe anapaswa kuheshimu kazi ya sekta zisizo rasmi. Wazimbabwe wanapaswa kuelewa kuwa Mugabe ni mzee na ni mtu anayetembea lakini ameshakufa,” aliongeza.

Gazeti la Harald la nchi hiyo limeripoti kuwa wamachinga wote wameondolewa mitaani na jeshi la polisi kutekeleza amri ya Rais.

Trump aitaka UNESCO kuacha ubaguzi
Serikali kudhibiti utoroshwaji wa Tanzanite