Kingo mshambuliaji wa mabingwa wa soka nchini England Leicester City, Riyad Mahrez amekata mzizi wa fitna na kueleza wapi anapotarajia kuelekea mara atakapofikiria kuondoka King Power Stadium.

Kiungo huyo mwenye umri wa miaka 25, ambaye alitajwa kuwa mchezaji bora wa msimu wa 2015/16 kupitia tuzo za chama cha wachezaji wa kulipwa nchini England (PFA), amesema zipo klabu mbili ama tatu ambazo huenda akafikiri kuzitumikia.

Mahrez alifanyiwa mahojiano na jarida la michezo ya nchini Ufaransa liitwalo (France Football) ambapo alisema klabu kama Real Madrid na FC Barcelona huenda zikawa suluhisho la yeye kuondoka King Power Stdium kwa sasa.

Alisema kila mchezaji mzuri na mwenye malengo ya soka lake, mara zote amekua akifikia kusonga mbele kwa kucheza mahala penye mafanikio na kwa upande wake anaamini Real Madrid na FC Barcelona ndio mahala sahihi pa kwenda.

“Ligi ya nchini England (Premier League) ni ligi bora na sisi ndio mabingwa watetezi hivyo ningependa kuendelea kuwa hapa kwa namna inavyowezekana. Lakini kama itatokea moja ya klabu ninazohitaji na zikaonyesha nia sitachelewa kufanya maamuzi.” Alisema Mahrez

Kauli hiyo ya Mahrez imezima fununu zilizokua zinaendelea dhidi yake za kutaka kusajiliwa na klabu ya Arsenal katika kipindi hiki cha majira ya kiangazi, na uchunguzi uliofanywa na kituo cha televisheni cha Sky Sports umebaini The Gunners hawakutuma ofa ya Pauni milioin 30 kwa ajili ya kiungo huyo kama ilivyokua inaripotiwa.

Kuhusu ushindani wa ligi kuu ambao ulianza kuonekana mwishoni mwa juma lililopita kwa kikosi cha mabingwa watetezi kukubali kufungwa mabao mawili kwa moja dhidi ya Hull City, Mahrez alisema hawana budi kuongeza juhudi ya kupambana na kufikia lengo la kuendelea kuwa bora.

“Tunafahamu hatuwezi kutwaa tena taji la England kwa msimu huu. Sisi sio Manchester United ama Chelsea,” Alisema.

“Lakini tunachokihitaji ni kutaka kuwa miongoni mwa timu ambazo zitapambana na kuonyesha uwezo wa kisoka katika ligi ya England, ili kuweka uwiyano wa mambo tuliyoyaonyesha msimu uliopita.

“Mara zote unapaswa kuthibitisha ubora wako kwa kuonyesha uwezo na kufikia malengo. Kwa sasa mashabiki wengi wanatarajia mambo makubwa kutoka kwetu. Na sisi hatuna budi kuthibitisha hilo kwa kurejesha fadhila kwao za kutuamini.” Aliongeza Mahrez.

Simba SC Yavunja Mkataba Na Janvier Besala Bokungu
Everton Kufuta Ndoto Za Moussa Sissoko