Kiungo wa Simba kutoka Zimbabwe, Justice Majabvi kwa mara ya kwanza amezungumzia sakata lake la kugoma kujiunga na wenzake kwenye safari ya Mwanza.
Majabvi ambaye ni mchezaji tegemeo wa Simba amekana madai ya kuandika waraka unaosema amechoshwa na maisha ya Simba.
“ Sijazungumza na waandishi wala kuandika chochote kama inavyozungumzwa. Mimi sio mtu wa kuzungumza ovyo. Hili ni suala langu na Simba. Nawasubiri waje tulitatue tatizo.”
Kiungo huyo ambaye ni mchezaji pekee wa Simba aliyecheza mechi zote kumi za Ligi Kuu Vodacom Tanzania Bara amesema madai yake ya msingi ni sehemu nzuri ya kuishi. Suala si sehemu ya gharama bali utulivu.
“ Mimi ni mtu wa familia. Si mnywaji wala mvutaji, sipendi starehe za usiku, nahitaji sehemu tulivu ya kuishi. Pale hotelini hakuna utulivu, kuna muingiliano mkubwa wa watu masaa yote. Pilika pilika haziishi. Huwezi kutuliza. “
“ Nachohitaji ni sehemu tulivu kwa ajili ya kuweza kuishi na familia yangu. Sehemu tulivu sio lazima iwe ya gharama. Simba walinionesha nyumba mbili. Moja Lamada ilikuwa ndogo na ya pili tulikuta imeshapangishwa.”
Majabvi amesema amekuwa akifuatilia suala la nyumba ya kuishi kwa muda sasa bila mafanikio. Kwa kuwa yeye sio mtu wa maneno ataendelea kuwasubiri Simba waje waka chini kulizungumzia suala lake